Habari Mseto

Drama mfereji uliokuwa ukizinduliwa na Gavana Kihika ukikataa kutoa maji kwa muda

Na WINNIE ONYANDO September 26th, 2024 1 min read

WANAKIJIJI waliachwa vinywa wazi kwa muda mfereji uliokuwa ukizinduliwa na Gavana wa Nakuru Susan Kihika ukikataa kutoa maji.

Katika video iliyosambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii, gavana huyo alisikika akimuuliza mama mmoja matatizo ambayo amepitia akitafuta maji safi.

“Umekuwa ukitembea kilomita ngapi kabla upate maji….. seven kilometers… alafu unakuja seven kilometers na maji. Sasa utakuwa unafungua maji kwako,” gavana huyo alisema.

“Haya basi hebu tufungue mfereji na wewe…”

Waliokuwa wakipiga vigelevele wakati Gavana Kihika na mama huyo wakifungua mfereji walisitasita kidogo maji yalipokataa kutoka kwenye mfereji huo.

Wakati huo, Bi Kihika pamoja na mama huyo walionekana waking’ang’ana kufungua mfereji huo wa maji bila mafanikio.

Hii ilifanya baadhi ya watu hasa wanaotumia mitandao mbalimbali ya kijamii wafikirie kuwa gavana huyo alikuwa akizindua mfereji usiotoa maji.

Hata hivyo, gavana huyo alielezwa na timu yake kuwa mfereji huo unafaa kufunguliwa kwa nguvu.

“Ooooh, tunafungua soft..na mimi na wewe tunafanya opposite. Na maisha si sasa imekuwa mzuri. Na unaona inatoa maji safi sana. Sasa mama hutateseka tena,” akasema gavana huyo huku watazamaji wakicheka.

Video hiyo imevutia makini ya watu wengi katika mitandao mbalimbali ya kijamii wengine wakimkashifu gavana huyo kwa kuzindua mfereji usiotoa maji.

Wengine walimtetea gavana huyo wakisema kuwa video hiyo ilikatwa na watu wakasambaza sehemu ambayo inaonyesha maji yakikataa kutoka kwenye mfereji.