Habari Mseto

Mkulima alia kufidiwa Sh3,000 kwa uharibifu wa Sh800,000 kutoka kwa wanyamapori

Na DAVID MUCHUI June 16th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

LICHA ya Rais William Ruto kuzindua hazina ya kuwalipa fidia wanaovamiwa au mali yao kuharibiwa kutokana na mzozo wa binadamu na wanyamapori ya Sh950 milioni, bado wengine wanalipwa kiwango cha chini.

Hazina hiyo ilizinduliwa mnamo Mei 26, 2025 kuhakikisha wakulima au wanaojeruhiwa wanalipwa fidia ya haraka.

Katika eneo la Igembe ya Kati, Kaunti ya Meru, baadhi ya waathiriwa wamelalamikia malipo duni huku wakipokea Sh3,000 pekee.

Mkulima Nancy Wanja alilipwa Sh3,000 pekee licha ya maafisa wa Shirika la Huduma kwa Wanyamapori (KWS) na wale wa kilimo kukadiria uharibifu uliotekelezwa na ndovu shambani mwake kuwa Sh800,000.

Waathiriwa wengine maeneo ya Kanjoo, Kinanduba, Ntukai, Kiruuyu pia walilamikia kuwa wamepokea fidia ya chini ikilinganishwa na hasara ambayo walipata shambani mwao kutokana na uvamizi wa wanyamapori.