31 waliokamatwa wakati wa maandamano ya kupinga kituo cha Ebola waachiliwa
WATU 31 waliokamatwa wakati wa maandamano ya Jumatatu dhidi ya mpango wa serikali wa kuanzisha kituo cha kutenga wagonjwa wa Ebola katika Kaunti ya Laikipia, jana waliachiliwa huru baada ya mashirika ya kutetea haki za binadamu kuingilia kati.
Waandamanaji hao walikamatwa wakati wa maandamano yaliyotikisa mji wa Nanyuki Juni 2 na baadaye kufikishwa mbele ya mahakama ya Nanyuki.
Wakiwa mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Daniel Ngayo, washukiwa 17 walikiri kosa la kufunga barabara za umma kwa kutumia mawe, magogo na magurudumu ya magari yaliyokuwa yakichomwa moto, kitendo kilichohatarisha usalama wa watumiaji wa barabara na kutatiza usafiri. Wengine 14 walikanusha mashtaka hayo.
Kesi hiyo ilisikizwa katika mahakama ya muda iliyowekwa ndani ya Kituo cha Polisi cha Nanyuki baada ya waandamanaji kuharibu majengo ya Mahakama ya Nanyuki wakati wa maandamano.
Waliohukumiwa baada ya kukiri kosa walitozwa faini ya Sh10,000 kila mmoja au watumikie kifungo cha mwezi mmoja gerezani iwapo wangeshindwa kulipa. Wale 14 waliokanusha mashtaka waliachiliwa kwa dhamana ya pesa taslimu ya Sh30,000 au Sh50,000 na mdhamini mmoja.
Akizungumza jana na wanahabari nje ya Kituo cha Polisi cha Nanyuki, wakili wa shirika la Sheria Mashinani, Derrick Maingi, alisema waandamanaji 27 walikuwa wameachiliwa asubuhi huku waliobaki wakitarajiwa kuachiliwa baadaye siku hiyo.
“Tulitafuta fedha kupitia Defenders Coalition na kufanikisha kuachiliwa kwa wale 14 waliokanusha mashtaka. Kwa wengine, tulizungumza na wasamaria wema ambao walikubali kulipa faini zao,” alisema Bw Maingi.
Kuachiliwa kwao kunajiri huku baadhi ya wakazi wa Nanyuki wakiahidi kuandaa maandamano mengine Jumanne ijayo kupinga mpango wa serikali wa kuanzisha kituo cha karantini katika Kambi ya Jeshi la Anga ya KDF Laikipia.
“Mimi ninawahimiza Wakenya kujiunga nasi Jumanne ijayo kwa sababu nchi ina changamoto nyingi zinazohitaji kushughulikiwa, na kuleta Ebola nchini hakupaswi kuwa mojawapo,” alisema mfanyabiashara wa Nanyuki, Marlin Ndegwa.
Wakati huo huo, mjadala kuhusu suala hilo umeendelea kushika kasi kisiasa. Waziri wa Afya Aden Duale alipuuzilia mbali maandamano hayo, akidai yalichochewa kisiasa na kuendeshwa na watu waliolipwa.
Kwa upande wake, aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alidai mpango huo una nia ya kisiasa na kuishutumu serikali ya Rais William Ruto kwa kulenga eneo la Mlima Kenya.
Naye Gavana wa Nyeri Mutahi Kahiga ametaka kusitishwa kwa mpango huo hadi mashauriano ya kina yafanywe na wadau wote. Alitaka Wizara ya Afya kuweka wazi ripoti zote za kiufundi, mazingira na usalama kuhusu kituo hicho.
Viongozi wa Laikipia pia wamepinga kwa kauli moja mradi huo wakisema ulipitishwa bila kushauriana nao wala jamii za eneo hilo.