Habari

Afisa aliyenaswa na mamilioni afutwa kazi

Na KEVIN CHERUIYOT June 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

GAVANA wa Nairobi Johnson Sakaja amemsimamisha kazi Afisa Mkuu wa Mipango Miji, Patrick Akivaga Analo, kufuatia kukamatwa kwake na Tume ya Maadili na Kupambana na Rushwa (EACC), baada ya kudaiwa kupatikana nna Sh65 milioni nyumbani kwake.
Katika taarifa jana, Sakaja alisema serikali ya kaunti itashirikiana kikamilifu na EACC ili kurahisisha uchunguzi wa madai ya rushwa na kupatikana kwa kiasi hicho kikubwa cha fedha.
“Ufisadi hauna nafasi katika utumishi wa umma. Kila afisa atawajibika binafsi kwa vitendo vyake,” alisisitiza Sakaja. Hata hivyo, aliwakumbusha wananchi kanuni ya katiba kwamba kila mtu hana hatia hadi ithibitishwe na mahakama
Analo aliachiliwa kwa dhamana ya Sh500,000 na kupigwa marufuku kuingia ofisini au kufikia stakabadhi za serikali uchunguzi ukiendelea. Dominic Mutegi, Mkurugenzi wa Udhibiti wa Maendeleo, atachukua nafasi yake kwa muda.
Sakaja pia alisitisha utoaji wa vibali vya ujenzi hadi kamati mpya ya mipango itakapoundwa upya..
Gavana aliahidi kuwa hakuna mtu atakayelindwa akigunduliwa kuhusika na ufisadi, na kwamba huduma za kaunti hazitasitishwa.