Shule zaendelea kufungwa wimbi la fujo likitanda
Wimbi la migomo, visa vya moto na vurugu za wanafunzi linaendelea kuzua hofu kubwa katika sekta ya elimu baada ya shule kadhaa za upili kufungwa jana katika maeneo mbalimbali nchini.
Zaidi ya shule 15 katika kaunti za Trans Nzoia, Nakuru, Bomet, Kericho, Narok, Kisii na Nyamira zimefungwa au wanafunzi kuruhusiwa kwenda nyumbani kutokana na vurugu, visa vya uchomaji mali na hofu ya migomo.
Shule ya hivi karibuni kuathiriwa ni Shule ya Upili ya Wasichana ya St Teresa’s Bikeke iliyoko Kiminini, Kaunti ya Trans Nzoia. Uongozi wa shule hiyo uliifunga kwa muda usiojulikana baada ya kupokea taarifa kuhusu mpango wa wanafunzi kufanya mgomo.
Mkuu wa shule hiyo, Eva Tsuma, aliomba wanafunzi waruhusiwe kwenda nyumbani kama hatua ya tahadhari. Mkurugenzi wa Elimu wa Kaunti ya Trans Nzoia, Pamela Akello, alithibitisha kufungwa kwa shule hiyo huku uchunguzi ukiendelea.
Hatua hiyo ilikuja siku moja tu baada ya wadau wa elimu katika kaunti hiyo kufanya mkutano wa dharura kujadili ongezeko la migomo mashuleni.
Katika eneo la South Rift, shule tano zimefungwa ndani ya siku mbili zilizopita. Kaunti ya Bomet imeshuhudia kufungwa kwa shule za Saseta Girls, Koiwo Boys na Tenwek Boys kutokana na hali ya sintofahamu. Shule ya Tengecha Girls katika Kaunti ya Kericho na Euro Ekulet Secondary School katika Kaunti ya Narok pia zimefungwa, huku bweni katika shule ya Euro Ekulet ikichomwa.
Nakuru ndiyo imeonekana kuathirika zaidi ambapo shule saba zimewatuma wanafunzi nyumbani kufuatia visa vya vurugu na moto. Miongoni mwa shule hizo ni Moi Forces Lanet, St Joseph’s Seminary Molo, Naivasha Girls, Marymount School, Utumishi Girls Senior School na Njoro Girls.
Matukio hayo yanafuatia mkasa wa moto katika Shule ya Utumishi Girls, Naivasha, uliosababisha vifo vya wanafunzi 16 mwishoni mwa mwezi Mei na kuibua maswali kuhusu usalama wa wanafunzi katika shule za bweni.
Mkurugenzi wa Elimu wa Nakuru, Victoria Mulili, amewataka wasimamizi wa shule kuimarisha huduma za ushauri nasaha na kufuatilia hali za wanafunzi kwa karibu ili kuzuia matukio mengine.
Katika eneo la Gusii, Shule ya Kisii ilifungwa Jumamosi baada ya wanafunzi kuzua vurugu siku ya kutembelewa na wazazi.
Shule ya Sironga Girls nayo ilifungwa baada ya wanafunzi kudai waruhusiwe kwenda nyumbani huku Sameta Boys na Masosa Secondary School zikishuhudia visa vya moto vilivyoharibu mabweni.
Ingawa hakuna majeruhi walioripotiwa katika baadhi ya matukio hayo, wadau wa elimu wanaonya kuwa ongezeko la migomo na moto linaashiria matatizo makubwa zaidi katika mfumo wa elimu.