Habari za Kitaifa

Ripoti yafichua sababu za wavulana wengi kukatiza masomo kuliko wasichana

Na MORAA OBIRIA May 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UMEWAHI kukutana na mvulana mdogo anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 10 akiomba ununue pipi au ndizi  barabarani wakati wanafunzi wengine wako shuleni? Je, umewahi kujiuliza kwa nini hayuko darasani?

Ripoti mpya imeonyesha kuwa Kenya inakabiliwa na changamoto kubwa ya elimu huku wavulana wengi wakiacha masomo kuliko wasichana, licha ya idadi yao kuwa ndogo nchini.

Kulingana na sensa ya mwaka 2019, wanaume ni asilimia 49.5 ya watu milioni 47.6 nchini huku wanawake wakiwa asilimia 50.5. Hata hivyo, utafiti wa shirika la Usawa Agenda unaonyesha kuwa wavulana watano kati ya 100 walio na umri wa kwenda shule hawapo shuleni, ikilinganishwa na wasichana wanne kati ya 100.

Ripoti hiyo yenye kichwa“Ni nini hali ya Usawa wa Jinsia katika Elimu Msingi yetu?” ilizinduliwa Jumanne na inaonyesha kuwa wavulana wako katika hatari kubwa ya kuacha shule katika familia zinazoongozwa na wanawake na hata zile zinazoongozwa na wanaume.

Mkurugenzi wa Usawa Agenda, Dkt Emmanuel Manyasa, alisema hali hiyo imeibua maswali mengi yanayohitaji utafiti zaidi.

“Tunazidi kuona wavulana wengi wakitoka shuleni. Hii ni hali inayohitaji kuchunguzwa kwa kina,” alisema.

Alisema baadhi ya wavulana katika maeneo ya uvuvi huamini wanaweza kupata pesa haraka kupitia kazi badala ya elimu. Aidha, katika maeneo ya Meru, biashara ya miraa imechangia wengi kuamini kuwa shule haina faida ya haraka.

“Wakati wa Covid-19, wavulana wengi waliingia katika kazi za boda boda na biashara ndogo ndogo. Walipoanza kupata Sh100 au Sh200 kwa siku, wengi hawakuona umuhimu wa kurejea shuleni,” alisema.

Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa mazingira ya kusoma bado yanawapendelea wavulana. Takriban asilimia 62 ya shule za wavulana zina zaidi ya masomo 12 ya mitihani, ikilinganishwa na asilimia 58.5 ya shule za wasichana.

Vilevile, shule nyingi za wavulana zina viwanja vya michezo na maktaba zaidi kuliko shule za wasichana.

Mwanzilishi wa Wakfu wa Chalan, Bi Margaret Koech, alisema changamoto zinazowakumba wavulana ni tofauti na zile za wasichana.

Kwa mujibu wake, wasichana huathiriwa zaidi na mimba za mapema na ndoa za utotoni, huku wavulana wengi wakiacha shule kutokana na umaskini na jukumu la kutafuta riziki kwa familia zao.

“Baadhi yao hulazimika kufanya kazi ili kusaidia ndugu zao au kujilipia karo,” alisema.

Bi Koech aliongeza kuwa matumizi ya dawa za kulevya, uhalifu, ukosefu wa ushauri nasaha, matatizo ya afya ya akili na ukosefu wa mifano bora ya kuigwa pia vinachangia wavulana wengi kuacha shule.

Mbunge wa Mandera South, Bw Abdul Haro, alisema Kenya haiwezi tena kudhani kuwa pengo la kijinsia katika elimu limezibwa kwa sababu tu ya ongezeko la wanafunzi wanaojiunga na shule.

“Tunapaswa kuhakikisha kila mtoto, mvulana au msichana, anapata nafasi salama ya kusoma na kubaki shuleni bila ubaguzi,” alisema.