Habari za Kaunti

Kisii yapata naibu gavana mpya


ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Bodi ya kuajiri Wafanyakazi na Utumishi wa Umma katika Kaunti ya Kisii, Elijah Obebo ameapishwa rasmi kama naibu gavana mpya wa gatuzi hilo.

Bw Obebo sasa atatwaa nafasi ya Dkt Robert Monda aliyeng’atuliwa mamlakani Machi mwaka huu, 2024 na Bunge la Seneti kwa matumizi mabaya ya mamlaka, miongoni mwa sababu zingine.

Hafla ya kumwapisha ilifanyika Jumatatu asubuhi, Julai 22, 2024 katika uwanja wa michezo wa Gusii.

Shughuli hiyo iliongozwa na maafisa kutoka idara ya mahakama na kushuhudiwa na Gavana Simba Arati.

Akizungumza baada ya uapisho wake, Bw Obebo aliahidi kuwa mwaminifu kwa bosi wake siku zote.

Pia, aliwahakikishia wakazi wa Kisii kwamba atajitahidi kuhakikisha anamsaidia Bw Arati kupambana na ufisadi.

“Nawahakikishia kuwa mtumishi mwema kwa bosi wangu. Pia, nitahakikisha matumizi mazuri ya rasilimali za umma,” Bw Obebo alisema.

Gavana Arati alimtaka msaidizi wake kutokubali watu wa nje kuwagonganisha na alimwomba awe mwaminifu wanapowahudumia wakazi wa Kisii.