Wawili wapigwa risasi na kuuawa Mbeere — wakilalamikia hospitali mbovu
WAANDAMANAJI wawili jana waliuawa kwa kupigwa risasi ghasia zilipozuka maandamano yakiendelea katika eneo la Ishiara, Kaunti ya Embu.
Watu wengine walipata majeraha ya risasi miguuni na kukimbizwa katika vituo mbalimbali vya afya kupokea matibabu. Wakazi walikuwa wakiandamana kulalamikia hali mbaya ya hospitali ya Ishiara, eneobunge la Mbeere Kaskazini.
Walilamikia ukosefu wa ambulensi, huduma duni, majengo yaliyochakaa na vyoo vilivyozibika huku wakitaka malalamishi yao yashughulikiwe na serikali ya Kaunti ya Embu.
Kamanda wa Polisi wa Mbeere Kaskazini Fredrick Odinga alikataa kuzungumzia suala hilo akisema kuwa bado alikuwa likizoni.
Wakati huo huo, wakazi wa Ngomeni, Kaunti ya Kitui wanaishi kwa hofu na kulazimika kulala kichakani kutokana na ukosefu wa usalama huku uhasama kati ya wafugaji wa kuhamahama na wakulima wa mazao ukizidi.
Zaidi ya familia 100 huhepa nyumba zao usiku unapoingia na kuenda kichakani ambako wanaishi kwa hofu pia ya kuvamiwa.
Wanalazimika pia kukaa ange wasiumwe na nyoka ambao pia ni wengi eneo hilo. Mnamo Jumatatu mchungaji wa ngamia Osman Hassan Ali alipigwa risasi na kufariki kwenye ranchi ya kibinafsi Kyso, Mwingi ya Kati.
Mauaji yake yamezidisha uhasama kati ya wakulima na wafugaji wa kuhamahama kwenye mpaka wa kaunti za Kitui -Tana River.
Wafugaji na wakulima wa mimea sasa wanalaumiana huku maafisa wa usalama wakiingilia uhasama huo japo ni dhahiri kuwa wamelemewa.
“Huwa tunalala kwenye kichaka nyakati za usiku na kuumwa na nyoka kwa sababu tunahofia majirani wetu wanaweza kujitokeza usiku na kutuvamia,” akasema Kambua Mutua, mzee wa kijiji katika eneo la Yumbandei.
Vijiji ambavyo vimeathirika sana ni Inyanzai, Mukavoo, Yumbandei na Kasiluni.