Wabunge wamtafuta Wandayi kuhusu miradi hewa ya kuunganisha stima
KAMATI ya Nishati ya Bunge la Kitaifa imezua maswali kuhusu miradi kadhaa ya kuunganisha stima mashinani katika maeneobunge kote nchini, akisema bado hawajapokea ufafanuzi bayana kutoka kwa Waziri wa Nishati Opiyo Wandayi.
Bw Wandayi alitarajiwa kufika mbele ya Kamati hiyo Jumanne kutoa maelezo kuhusu miradi iliyokwama.
Hata hivyo, alikosa kufika huku Kamati ikifahamishwa aliandamana na Rais William Ruto nchini Italy.
Mwenyekiti wa Kamati David Gikaria alisema: “Nilimwona Wandayi akiwa ameketi katika mkutano aliohudhuria Rais Italia.”
“Kama Bunge, tuna tatizo kwa sababu Serikali sasa inaadhiri ratiba yetu,” alisema Bw Gikaria.
Bw Wandayi alitarajiwa kufafanulia wabunge sababu ya miradi hiyo kukosa kuanzishwa licha ya kuzinduliwa kupitia hafla za ngazi za juu.
Bw Gikaria alisema huku baadhi ya maeneo yakiunganishiswa stima hadi asilimia 70, sehemu nyingine zimesalia chini asilimia 20.
Mbunge wa Awendo, Walter Owino, alisema miradi iliyokwama imegeuka kero kwa azma za kuchaguliwa tena kwa wabunge.
“Waziri anapaswa kuja atueleze iwapo anatatizwa na nani anamtatiza kwa sababu mradi huu utasambaratisha azma ya kuchaguliwa tena kwa watu wengi,” alisema, akirejelea mradi uliozinduliwa katika eneobunge lake miaka miwili iliyopita.
“Rais huzungumza kuuhusu kila anapozuru eneo hilo, akisema hela zimetengwa, lakini hakuna kinachofanyika,” alisema.
Mbunge wa Nambale, Geoffrey Mulanya alisema hana la kuwaeleza watu wa eneobunge lake.
“Tuache mzaha. Nitawaeleza nini wakazi wa eneobunge langu katika azma yangu ya kuchaguliwa tena?” Aliuliza.
Mbunge wa Nyatike, Tom Odege, alisema miradi mingi huzinduliwa kwa maonyesho tu.
“Unakuta waziri amewasili na lori na malighafi, lakini mara tu anapoondoka, malighafi inatoweka vilevile. Ni nani tunapumbaza?” Aliuliza.
Wiki iliyopita, Katibu wa Wizara ya Nishati, Alex Wachira, alishutumiwa na wabunge kwa kuzindua miradi mikubwa kwa mbwembwe, kisha vifaa vinatoweka baada ya maafisa kuondoka eneo husika.
Kamati sasa inaitisha ufafanuzi kuhusu iwapo ucheleweshaji huo unatokana na upungufu wa ufadhili kutoka kwa serikali au washiriki wa maendeleo kukosa kutimiza majukumu yao kifedha.