Habari za Kitaifa

Baba apewa mtoto baada ya vita vya kisheria kuhusu ‘ubebaji mimba’

Na SAM KIPLAGAT April 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIA mmoja wa Amerika aliyetambuliwa kama A.M, amezua mjadala wa kisheria nchini baada ya kuja Kenya mwaka 2024 akiwa na lengo la kupata mtoto kupitia mpango wa uzazi wa kiteknolojia wa kubeba mimba.

Alifanya makubaliano na mwanamke wa Kenya, C.A.O, ambapo alikubali kumbebea mimba na kisha kuachilia haki zote za uzazi kwa mtoto huyo baada ya kuzaliwa.

Mtoto alizaliwa Januari 28, 2025, na A.M akawasilisha ombi mahakamani akitaka kutambuliwa kisheria kama mzazi na kupewa ulezi kamili ili aweze kurejea Amerika.

Aliwasilisha ushahidi ambao ni pamoja na matokeo ya DNA yaliyothibitisha yeye ndiye baba wa mtoto huku mama mbeba mimba akiwa hana uhusiano wa kijenetiki na mtoto huyo.

Hata hivyo, mahakama ya awali ilikataa kumpa ulezi, ikizingatia maslahi bora ya mtoto chini ya Katiba ya Kenya Ibara ya 53 na Sheria ya Watoto.

Mahakama iliamua kuwa kutokana na umri mdogo wa mtoto, ni vyema akae chini ya malezi ya “mama”, na kumtaka A.M amkabidhi C.A.O mtoto huyo.

Uamuzi huo uliibua mjadala mpana kuhusu mapendeleo ya kijinsia katika kesi za ulezi, ambapo mara nyingi mahakama huonekana kupendelea upande wa mama, hata pale ambapo hakuna msingi wa kibayolojia au kisheria.

A.M alipinga uamuzi huo katika Mahakama Kuu, ambayo baadaye ilibatilisha uamuzi wa mahakama ya chini.

Jaji Patricia Nyaundi alieleza kuwa ukosefu wa sheria mahsusi kuhusu uzazi wa kubeba mimba nchini haupaswi kunyima mtu haki ya kuwa mzazi.

“Mpaka pale sheria itakapowekwa, jukumu litabaki kwa mahakama kuhakikisha hakuna mtu, mwanaume au mwanamke – anayenyimwa haki ya uzazi ambayo teknolojia imewezesha,” alisema jaji huyo.

Mahakama ilibaini kuwa hakuna ushahidi unaoonyesha A.M ni hatari kwa mtoto, na ripoti ya Idara ya Huduma za Watoto ilipendekeza apewe ulezi.

Hatimaye, A.M alipewa mamlaka kamili ya ulezi, na Msajili wa Watu akaagizwa kutoa cheti cha kuzaliwa kinachomtambua kama baba wa mtoto.

Kesi hii inaangazia pengo la kisheria kuhusu uzazi wa kubeba mimba nchini Kenya, pamoja na changamoto wanazokumbana nazo wanaume wanapotafuta haki za ulezi hasa katika mipango isiyo ya kawaida ya uzazi.