Jinsi suala la ‘kuachiana ngome’ linavyogonganisha vichwa ndani na nje ya serikali
SWALI la ni nani atakuwa na wagombea wepi linaondokea kuwa kikwazo kikuu katika kuunda miungano ya kisiasa Kenya kuelekea katika uchaguzi mkuu wa 2027, huku mzozo huo ukitokota ndani ya Serikali Jumuishi na pia muungano unaosukwa na upinzani.
Mpango wa kuachiana maeneo ya uchaguzi ili kuepuka kugawanya kura sasa unageuka kuwa chanzo cha mvutano, vyama vikilazimika kuchagua kati ya kulinda ngome zao za jadi au kuruhusu ushindani huru.
Ndani ya Serikali Jumuishi inayoongozwa na Rais William Ruto, mvutano umeibuka kati ya chama tawala cha UDA na chama cha ODM kinachoongozwa na Oburu Oginga, ambapo ODM inataka ngome zake za jadi ziheshimiwe, huku UDA ikisisitiza mpango wa kitaifa wa ushindani wa wazi.
Katika upinzani pia, hali ni tata. Viongozi kama Martha Karua wa PLP na mgombea urais wa Jubilee Fred Matiang’i wanapinga vyama kuhifadhiwa maeneo ya uchaguzi, wakitaka ushindani wa wazi badala ya makubaliano ya juu kwa juu.
Chama cha Jubilee, ambacho zamani kilikuwa na nguvu katika Mlima Kenya chini ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta, sasa kinakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa chama cha DCP kinachoongozwa na aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua.
Bw Gachagua amekuwa akisisitiza kuwa siasa za Mlima Kenya lazima zisimamiwe na viongozi wake wa ndani, huku Matiang’i akijaribu kujipenyeza katika eneo hilo kupitia mikutano ya kisiasa na wito wa umoja.
Bi Karua, kwa upande wake, amekuwa sauti kuu ya kupinga makubaliano ya vyama kuachiana ngome, akisema hatua hii inaweza kudhoofisha demokrasia na kuwanyima wananchi haki ya kuchagua viongozi wao.
“Tunataka kila mgombea apimwe na wananchi, si kuamuliwa nyuma ya milango,” anasema Karua, akisisitiza mfano wa NARC mwaka wa 2002 iliyomuingiza Rais Mwai Kibaki madarakani.
Hata hivyo, mazingira ya sasa ya kisiasa yamebadilika kutokana na ugatuzi na kuongezeka kwa ushindani wa viti vingi vinavyowaniwa, hali inayofanya utekelezaji wa kutengea vyama ngome kuwa mgumu zaidi.
Wachambuzi wa siasa wanaonya kuwa bila mfumo wa wazi, upinzani unaweza kugawanyika zaidi kutokana na uwepo wa wagombea wengi wa urais na ubunge.
Mizozo kuhusu hatua hii imeonekana zaidi katika Mlima Kenya, ambapo UDA, DCP na Jubilee zote zinawania ushawishi.
Kwa Ruto, kudhibiti eneo hilo ni muhimu kwa mustakabali wake wa kisiasa, huku Gachagua akilichukulia kama nguzo ya nguvu zake katika mazungumzo ndani ya upinzani.
Katika Serikali Jumuishi, UDA imekataa wito wa ODM wa kugawana maeneo, ikisisitiza kuwa itakuwa na wagombea wa viti vya uchaguzi nchi nzima.
Katibu Mkuu wa UDA, Hassan Omar amesema chama hicho hakitafanya makubaliano ya kugawana maeneo ya uchaguzi na ODM.
UDA imekuwa ikifanya uchaguzi wa mashinani katika kaunti mbalimbali, ikiwemo ngome za ODM kama Kisumu, Siaya na Migori, hatua ambayo imefasiriwa kama changamoto ya moja kwa moja kwa ushawishi wa ODM katika maeneo yake ya jadi.
Kwa upande wake, ODM imejibu kwa kuongeza kasi ya uhamasishaji mashinani, ikipanga mikutano ya vijana na kuimarisha miundo ya chama kulinda maeneo yake ya kisiasa.
Hali hii imeleta mwelekeo ambapo vyama hivyo vinashirikiana serikalini lakini vinashindana vikali chini mashinani, hali inayozidisha mvutano wa kimkakati kuelekea 2027.
Wachambuzi wanasema mkakati wa Rais Ruto wa kuunda miungano huku pia akipanua ushawishi wa UDA unakabiliwa na hatari ya kuvuruga mshikamano wa kisiasa.
Hasa kwa vyama vidogo ndani ya Kenya Kwanza, wasiwasi umeongezeka kuhusu iwapo vitaruhusiwa kusimamisha wagombeaji katika ngome zao za jadi au vitalazimika kuachia UDA au ODM.
Tayari, baadhi ya viongozi wameanza kuchukua misimamo ya kisiasa mapema. Kiongozi wa PAA na Spika wa Seneti Amason Kingi amesema yuko tayari kuunga mkono wagombeaji wa UDA katika uchaguzi ujao, hatua inayoashiria mabadiliko ya kisiasa katika muungano huo.
Hata hivyo, mpango wa Ruto wa kuunganisha vyama chini ya UDA unakutana na upinzani kutoka kwa viongozi wanaotaka kubaki na vyama vyao.
Miongoni mwao ni Spika wa Bunge, Moses Wetang’ula, ambaye anaendelea kusisitiza umuhimu wa kudumisha Ford Kenya.
Kurudi kwa chama cha ANC baada ya uamuzi wa mahakama kubatilisha muungano wake na UDA kumeongeza changamoto zaidi katika mwelekeo wa siasa hizi.
Hii imepatia ANC nafasi mpya ya kujadiliana kuhusu ushawishi wake ndani ya muungano wa serikali.
Hata hivyo, uhai mpya wa ANC umemweka mwanzilishi wake Musalia Mudavadi katika nafasi ngumu ya kisiasa, baada ya baadhi ya viongozi wake kuingizwa katika uongozi wa UDA.
Miongoni mwao ni Gavana wa Lamu Issa Timamy, aliyepanda ngazi hadi naibu mwenyekiti wa pili wa UDA, pamoja na Omboko Milemba na Kelvin Lunani ambao walishushwa vyeo ndani ya muundo mpya wa chama.