Habari za Kitaifa

Damu changa zinazotishia vigogo wa kisiasa 2027

Na MOSES NYAMORI April 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKIUNGWA mkono na vijana wa Gen-Z wanaozidi kuwa wakakamavu kwa usemi, sura mpya za wanasiasa zinajitokeza kama wagombea muhimu katika kinyang’anyiro cha 2027.

Kundi hilo jipya la viongozi tayari linashinikiza mabadiliko ya kizazi ndani ya vyama vyao kwa kushindana moja kwa moja na vigogo wakongwe au kuamua kuanzisha mkondo wao tofauti kisiasa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Kuinuka katika umaarufu kitaifa kumewaweka katika nafasi ya kuwania nyadhifa kuu za uchaguzi, ukiwemo urais.

Huku tasnia ya kisiasa ikizidi kubadilika, vigogo wa tangu jadi kisiasa, wanakodolea macho kudidimia kisiasa nao wanasiasa wachanga wakiwakabili ana kwa ana.

Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna na Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro ni miongoni mwa wanasiasa vijana waliojitokeza zaidi nchini. Wote wawili wametajwa miongoni mwa wagombea ambao huenda wakawania kiti cha urais 2027.

Wengine ambao wamegeuka wanasiasa mashuhuri kuelekea chaguzi wanajumuisha Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, Seneta wa Nyandarua, John Methu, Mwakilishi Mwanamke Kirinyaga, Njeri Maina, Mbunge wa Nyali, Mohammed Ali, na naibu kinara wa DCP Cleophas Malala.

Bw Sifuna ndiye kinara wa Linda Mwananchi, kundi linalokua kwa kasi lililojitenga kutoka ODM ambalo linapinga serikali ya muungano na uongozi wa Dkt Oburu Oginga.

Bw Sifuna ametajwa kama anayeweza kuwa mgombea urais wa kundi hilo hatua itakayobadilisha mipangilio ya ODM na mwelekeo wa kinyang’anyiro cha 2027.

Kambi hiyo inayoonekana kuwiana vyema na wapigakura vijana, imeshiriki misururu ya mikutano ya hadhara kote nchini ikijitahidi kuzindua mchango wa umma, kurejesha utawala wa kikatiba na kuunganisha uongozi wa kisiasa na uhalisia mashinani.

Bw Nyoro, 40, kwa upande mwingine, amevutia umaarufu kama mbunge mwenye ufasaha na anayeoongozwa na sera.

Japo angali mwanachama wa UDA, ameibuka kuwa moja kati ya wakosoaji sugu wa serikali ya Kenya Kwanza.

“Viongozi kama vile Sifuna, Nyoro na Babu wanaashiria kuinuka kwa kizazi cha wahusika stadi kisiasa,” anasema mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Moi, Profesa Masibo Lumala.

Anasema Sifuna, hasa, anajitokeza kwa njia ya kipekee sio tu kwa azma, bali weledi kisiasa kimaksudi huku akijiweka kwenye nafasi ya kugombea urais 2027.

“Nguvu za Nyoro zipo kwenye uadilifu wa tabaka tawala na msingi wa kisera, huku Babu Owino akijivunia ngome imara inayoegemea uanaharakati unaounda simulizi za siasa za maeneo ya mijini.”

“Kwa pamoja, wataathiri ajenda na uhamasishaji 2027. Hata hivyo, ugombea urais wa Sifuna unapima kwa njia ya kipekee iwapo uwaniaji unaoendeshwa na ujumbe na vijana unaweza kubadilisha mwonekano na uwiano kuwa uwezo wa kuchaguliwa kitaifa katika mpangilio wa kisiasa nchini,” anafafanua Profesa Masibo.