Habari za Kitaifa

HABARI ZA HIVI PUNDE: Mgomo wa sekta ya uchukuzi waahirishwa kwa siku saba

Na BENSON MATHEKA May 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MGOMO wa sekta ya uchukuzi uliokuwa umeingia siku ya pili umeahirishwa kwa muda wa siku saba ili kutoa nafasi kwa mazungumzo kati ya serikali na viongozi wa sekta hiyo.

Tangazo hilo lilitolewa na Waziri wa Uchukuzi Kipchumba Murkomen baada ya mkutano na viongozi wa sekta ya uchukuzi uliohudhuriwa pia na Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi.

Bw Murkomen alisema serikali imekubaliana na viongozi hao kuendelea na mazungumzo katika ngazi za juu ili kutafuta suluhu ya malalamishi yaliyoibuliwa na wadau wa uchukuzi.

Hata hivyo, viongozi wa sekta hiyo walionya kuwa mgomo huo unaweza kurejea baada ya siku saba iwapo serikali haitazingatia matakwa yao.

Walisema wamekubali kusitisha mgomo huo kwa muda ili kuruhusu mazungumzo kuendelea lakini wakasisitiza kuwa wanataka hatua za haraka kuchukuliwa kuhusu changamoto zinazowakabili.

Mgomo huo uliokuwa umeathiri shughuli za usafiri katika maeneo mbalimbali nchini ulianzishwa kupinga kupanda kwa bei ya mafuta na gharama nyingine za uendeshaji katika sekta ya uchukuzi.

Katika baadhi ya miji, wasafiri walikwama huku magari ya uchukuzi wa umma yakionekana machache barabarani kutokana na maandamano ya wahudumu na madereva.

Serikali sasa inatarajiwa kutumia muda huo wa siku saba kufanya mashauriano zaidi na wadau wa sekta hiyo ili kuzuia kurejea kwa mgomo huo ambao unaweza kuathiri uchumi na shughuli za kawaida nchini.