Habari za Kitaifa

Ong’ondo Were hakucheka na wapinzani wa Raila, ODM

Na CECIL ODONGO May 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MBUNGE wa Kasipul Ongóndo Were ambaye aliuawa kikatili jijini Nairobi Jumatano usiku alikuwa mcheshi na hakufichua ufuasi  na uaminifu wake kwa Kinara wa ODM Raila Odinga.

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, mbunge huyo ambaye  alikuwa akihudumu muhula wake wa pili, alipigwa risasi na mtu aliyekuwa amebebwa kwenye pikipiki katika mzunguko wa barabara ya Ngong’.

Bw Odinga mwenyewe alimwomboleza Bw Were huku akisema kifo chake ni pigo ikizingatiwa ni kiongozi ambaye alithamini utoaji huduma kwa watu waliomchagua.

“Tumepoteza mwana shujaa wa kwetu Mheshimiwa Charles Ongóndo ambaye ameaga. Ameuawa kinyama kwa kupigwa risasi na mhuni Nairobi jioni hii. Pumzika kwa amani Mheshimwa Charles Ong’ondo Were. Nenda salama Mfalme wa Kusini,” akaandika Bw Odinga.

Marehemu alifahamika miongoni mwa wabunge wenzake kama Sir Charles ama Ogai ma Milambo (Mfalme wa Kusini) akijirejelea kama mwanasiasa ambaye eneo lote la Nyanza Kusini lilikuwa chini ya uongozi wake.

Kando na Bw Odinga,  Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, Mbunge wa Suba Kaskazini Millie Odhiambo miongoni wa wabunge na wanasiasa walimwomboleza wengi wakitambua ucheshi wake na uaminifu wake kwa ODM.

“Mimi ndiyo mtu wa mkono ya baba hata kama mambo yaliharibika 2022, bado tuko naye. Raila si mtu wa kutusiwa na ukimtusi unaenda mbaya wala huwezi kumrithi katika uongozi wa hapa Nyanza,

“Mtu hawezi kutoka tu na kusema anaweza kurithi nafasi ya Raila kwa sababu mwenyewe ni asasi,” alisema mnamo Disemba 18, 2022 akiwa katika Kaunti ya Homa Bay.

Mnamo Oktoba 20 2023, Bw Were aliwaongoza wafuasi wake kuondoka kwenye  hafla ya maadhimisho ya Mashujaa kwenye eneobunge lake akilalamika kuwa Raila alidharauliwa na jina lake halikuwa likitajwa na waliokuwa wakiongoza sherehe hiyo.

Baada ya uchaguzi mkuu wa 2022, alikuwa kati ya viongozi wa upinzani ambao walikuwa wakijiunga na Bw Odinga kwenye maandamano ya kupinga utawala wa Rais Ruto.

Kinaya ni kwamba baada ya Raila kujiunga na Rais Ruto alibadili wimbo na alikuwa kati ya waliokuwa wakikosoa viongozi wengine wa Azimio na kusema vijana wa Nyanza hawakuumbiwa kuandamana tu bila kupewa maendeleo.

“Mimi mambo ya ODM na Baba inafanya nisilale. Hata mimi siku nitapumzika  nawaomba watu wa chama wafunike jeneza langu kwa bendera ya chama cha ODM na mje kwa fujo,” akasema Bw Were.

Alikuwa akiongea kwenye Kaunti ya Migori wakati wa mazishi ya Philip Makabongó ambaye alikuwa mwenyekiti wa ODM Kaunti ya Migori mnamo Januari 12, 2024.

Kabla ya Serikali Jumuishi, Bw Were alikuwa akikwaruzana na Katibu katika Wizara ya Usalama wa Ndani Raymond Omollo ambaye alikuwa mwandani wa Rais Ruto katika Kaunti ya Homa Bay.