Habari za Kitaifa

Pendekezo la kutumia droni kufuatilia polisi wakati wa maandamano lazua mjadala

Na ERIC MATARA May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

PENDEKEZO la Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) la kutumia teknolojia, ikiwemo droni, kufuatilia mienendo ya polisi wakati wa maandamano limezua mjadala mkali miongoni mwa wadau wa usalama na viongozi wa kisiasa.

Mpango huo unajiri wakati Huduma ya Kitaifa ya Polisi inakabiliwa na uchunguzi mkali kufuatia madai ya matumizi ya nguvu kupita kiasi, kukosa na kuchelewa kuwajibika katika hali za dharura na mapungufu katika ukusanyaji wa ushahidi, hasa wakati wa maandamano yanayokumbwa na fujo.

Katika miaka miwili iliyopita, polisi wamekuwa wakilaumiwa kwa ukatili wakati wa maandamano yaliyoongozwa na vijana kote nchini.

Akizungumza kuhusu pendekezo hilo, Mkurugenzi wa Ukaguzi, Ufuatiliaji na Huduma za Kuzuia katika IPOA, Munene Mugambi, alisema mamlaka hiyo inachunguza uwezekano wa kutumia teknolojia kama droni kufuatilia mwenendo wa maafisa wa polisi wakati wa maandamano na operesheni nyingine, huku nchi ikielekea uchaguzi mkuu ujao.

“Tunataka kutumia teknolojia kufuatilia mienendo ya maafisa wa polisi. Hii sio tu kutafuta makosa, bali pia kutambua wale wanaotekeleza wajibu wao kwa weledi,” alisema Mugambi.

Wabunge waliokutana Mombasa tayari wameunga mkono pendekezo hilo, wakisema litasaidia kuongeza uwajibikaji wa polisi kabla ya uchaguzi wa 2027.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama ya Bunge la Kitaifa, Gabriel Tongoyo, alisema wanaunga mkono matumizi ya teknolojia, lakini wakataka ufafanuzi kuhusu namna itakavyotekelezwa.

Hata hivyo, wabunge walisisitiza umuhimu wa IPOA kufanya tathmini ya kina ya hatari zinazoweza kujitokeza kabla na baada ya uchaguzi.

Mwakilishi wa Wanawake wa Nakuru, Liza Chelule, alisema maandalizi ya mapema ni muhimu kutokana na historia ya uchaguzi nchini inayohusishwa na mvutano.

Pendekezo hilo limepokelewa kwa hisia mseto huku Kamishna wa IPOA, Annette Mudola Mbogo, akisema droni zinafaa zaidi kutumika katika matukio yaliyopangwa.

Mbali na droni, IPOA pia inapanga kutumia kamera za mwilini, CCTV na vifaa vya kidijitali kurekodi matukio, hatua inayolenga kuimarisha ukusanyaji wa ushahidi na uwajibikaji.

“Teknolojia hizi zitafanya iwe vigumu kupotosha ushahidi na kuboresha uchunguzi,” alisema.

Hata hivyo, mtaalamu wa masuala ya usalama David Ngugi alionya kuwa gharama ya teknolojia kama droni ni kubwa na inaweza kuwa changamoto kwa serikali kuipata.

Mbunge wa Teso Kaskazini Oku Kaunya alisema kuwa ingawa droni zinaweza kusaidia katika operesheni zilizopangwa, hazifai sana katika matukio ya ghafla kama mashambulizi ya wahalifu.

Kwa upande wake, Mbunge wa Homa Bay Mjini Peter Kaluma alionya kuhusu hatari ya kuwafanya polisi kuwa waoga kufanya maamuzi muhimu ikiwa watahisi wanachunguzwa kila wakati.

“Tunahitaji kusawazisha haki za binadamu na jukumu la polisi kulinda usalama wa taifa,” alisema Kaluma.

Kwa mujibu wa takwimu za IPOA, maafisa 3,988 wa polisi kwa sasa wanachunguzwa kwa tuhuma za utovu wa nidhamu, huku 47 pekee wakiwa wamepatikana na hatia.

Baadhi ya waliohukumiwa wanahusishwa na maandamano ya vijana ya mwaka 2024 yaliyopinga Mswada wa Fedha.

Mugambi alisema uchunguzi huo unahusisha kesi za vifo, majeraha makubwa, makosa ya kingono na ukiukaji wa haki za binadamu.

Licha ya juhudi hizo, IPOA inakabiliwa na changamoto za ufadhili na rasilimali ambazo zinapunguza ufanisi wake.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2011, IPOA imekuwa ikichunguza malalamiko ya mauaji ya kiholela, mateso na unyanyasaji unaofanywa na polisi.