Siasa

Jinsi siasa za Kenya zinavyorudia historia ya kulipiza kisasi

Na SAMWEL OWINO May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BAADA ya muungano wa National Rainbow Coalition (NARC) chini ya uongozi wa marehemu Mwai Kibaki kushinda na kumaliza utawala wa miaka 40 wa Kenya African National Union (KANU), hali ya kisiasa iligeuka na kuibua kile kilichoonekana kama siasa za kulipiza kisasi.

Kulikuwa na shinikizo kubwa kutoka kwa baadhi ya wanasiasa kumkamata aliyekuwa Rais Daniel arap Moi kwa madai ya makosa aliyofanya wakati wa utawala wake wa miaka 24.

Aliyekuwa Waziri wa Sheria na Masuala ya Katiba, Kiraitu Murungi, aliwahi kufichua kuwa mashtaka dhidi ya Moi tayari yalikuwa yameandaliwa, na kilichosubiriwa ulikuwa ni wakati mwafaka wa kuyatekeleza.

Mpango huo haukuishia hapo tu; kulikuwa pia na pendekezo la kumtimua Moi katika makazi yake ya kifahari ya Kabarnet Gardens na kumpatia aliyekuwa Makamu wa Rais Kijana Wamalwa.

Hata hivyo, Rais Kibaki aliingilia kati na kusitisha hatua hizo.

Badala yake, alielekeza kuwa hati miliki ya makazi hayo ichakatwe na kuwekwa kwa jina la Moi.

Kulingana na Murungi, Kibaki hakutaka taifa liingie katika siasa za kisasi dhidi ya mtangulizi wake.

Kwa mujibu wa Murungi, uongozi huambatana na shinikizo kutoka pande mbalimbali zilizo na ajenda tofauti na jukumu la kiongozi ni kusikiliza na kusawazisha maslahi hayo.

Miaka kadhaa baadaye, mjadala huo umeibuka tena.

Seneta wa Nandi, Samson Cherargei, ameibua hoja ya kutaka kupitia upya marupurupu ya aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta.

Hatua hiyo imechochewa na kuendelea kwa Kenyatta kushiriki siasa, ikiwemo kukosoa serikali ya William Ruto na hata kuunga mkono wagombea kuelekea uchaguzi wa 2027.

Kikatiba, chini ya Ibara ya 38, kila raia ana haki ya kushiriki katika shughuli za kisiasa.

Kenyatta mwenyewe amesisitiza kuwa hana nia ya kugombea wadhifa wowote, bali ana haki ya kushiriki siasa kama mwanachama wa chama chake.

Akijibu wakosoaji wake, Kenyatta alirejelea historia ya Moi, akisema kuwa hakuwahi kuzuiwa kushiriki siasa hata baada ya kustaafu.

Hoja ya kuvuliwa marupurupu imeibua upya mjadala wa siasa za kulipiza kisasi, ambazo zimekuwa sehemu ya historia ya siasa za Kenya.

Wataalamu wa siasa wanaonya kuwa hatua hiyo inaweza kuwa na athari za kisiasa, hasa kwa Rais Ruto ambaye anajiandaa kwa uchaguzi wa 2027.

Katika eneo la Mlima Kenya lililo na kura nyingi, hatua yoyote inayoweza kuonekana kumlenga Kenyatta inaweza kuzua mvutano mpya wa kisiasa.

Aidha, upinzani unaweza kutumia hali hiyo kama silaha ya kisiasa dhidi ya serikali.

Sheria ya Mafao ya Marais Wastaafu ya mwaka 2013 inawapa marais waliostaafu marupurupu makubwa, ikiwemo malipo makuu, pensheni ya kila mwezi, magari, wafanyakazi na bima ya afya.

Hata hivyo, Bunge lina uwezo wa kuwanyima mafao hayo iwapo watapatikana na hatia ya kukiuka Katiba au kushiriki katika shughuli za kisiasa kwa namna inayokiuka masharti ya sheria.

Katika mwaka uliopita, wabunge pia walitishia kuwanyima mafao viongozi wengine wastaafu kama Kalonzo Musyoka, David Maraga na Justin Muturi kwa kushiriki maandamano ya kupinga serikali.

Wabunge kama Farah Maalim na Silvanus Osoro walisisitiza umuhimu wa kupitia upya sheria hizo ili kuhakikisha viongozi waliostaafu hawapati marupurupu huku wakiendelea na siasa hai.

Hata hivyo, kwa kuzingatia mgawanyiko wa kisiasa uliopo, ikiwa ni pamoja na makundi ndani ya ODM na vyama vingine, inakuwa vigumu kwa serikali kupitisha hoja kama hiyo kwa sasa.

Mjadala huu unaonyesha jinsi siasa za Kenya zinavyoendelea kuathiriwa na historia ya kulipiza kisasi, huku viongozi wakilazimika kusawazisha maslahi ya kisiasa na utulivu wa taifa.