Serikali ya Ruto yaibuka ghali zaidi kuwahi kushuhudiwa katika historia ya Kenya
RAIS William Ruto anaongoza ofisi ya urais inayogharimu mlipa ushuru zaidi kuliko ilivyowahi kushuhudiwa nchini, huku matumizi yake ikitarajiwa kufyonza takribani Sh100 bilioni ifikapo mwisho wa mwaka huu wa kifedha.
Kwa mujibu wa takwimu kutoka Wizara ya Fedha, Mdhibiti wa Bajeti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, matumizi ya ofisi ya urais chini ya Ruto yamefikia Sh88.8 bilioni chini ya miaka minne, karibu sawa na Sh89.9 bilioni zilizotumika katika kipindi chote cha miaka 10 cha utawala wa Uhuru Kenyatta.
Uchambuzi huo unaonyesha kuwa matumizi hayo yatafikia Sh100 bilioni ifikapo Juni 30, yakionyesha ongezeko kubwa la gharama za kuendesha serikali kuu.
Katiba ya mwaka 2010 iliunda Urais kama taasisi moja yenye idara mbalimbali zinazosimamia shughuli za serikali kuu.
Katika utawala wa sasa, Urais unajumuisha Afisi ya Utendaji ya Rais, Ofisi ya Naibu Rais, Ofisi ya Mkuu wa Mawaziri na idara za masuala ya Bunge na Baraza la Mawaziri.
Kwa upande wa utawala wa Kenyatta, pia kulikuwepo na Ofisi ya Mama wa Taifa pamoja na ofisi ya Marais wastaafu.
Takwimu zinaonyesha kuwa matumizi ya Urais yameongezeka kwa kasi chini ya utawala wa Rais Ruto.
Bajeti imepanda kutoka asilimia 0.44 ya bajeti ya taifa mwaka 2021/22 hadi asilimia 0.77 ya bajeti ya sasa ya Sh4.2 trilioni.
Katika kipindi cha miaka mitatu na miezi tisa ya utawala wa Ruto, asilimia 93.7 ya matumizi yote sawa na Sh83 bilioni yameelekezwa katika matumizi ya kawaida kama mishahara, safari, mafuta na shughuli za kiutawala.
Hali hii imeibua mjadala kuhusu matumizi makubwa ya fedha katika shughuli zisizo za maendeleo.
Ikulu imeongoza kwa matumizi makubwa zaidi, ikitumia Sh36.3 bilioni, ikifuatiwa na Afisi ya Utendaji ya Rais iliyotumia Sh35.1 bilioni.
Ofisi ya Naibu Rais Kithure Kindiki imetumia Sh12.5 bilioni, huku Ofisi ya Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi ikitumia Sh3.3 bilioni.
Katika mwaka huu wa kifedha, bajeti ya Urais imeongezwa hadi Sh32.2 bilioni kupitia marekebisho ya bajeti, huku Ikulu ikiongezewa Sh8.9 bilioni.
Mishahara ya wafanyakazi wa Ikulu pekee itagharimu Sh3.6 bilioni.
Serikali inatetea matumizi hayo ikisema jukumu kuu la Urais ni kuratibu shughuli za serikali na kuhakikisha utekelezaji wa sera na maamuzi muhimu.
Hata hivyo, wachambuzi wanasema ongezeko la matumizi ya kawaida linaibua maswali kuhusu uwiano kati ya gharama na matokeo.
Katika utawala wa Kenyatta, matumizi ya Urais yaliongezeka kutoka Sh4.5 bilioni mwaka 2012/13 hadi Sh12.9 bilioni mwaka 2021/22.
Kwa jumla, alitumia Sh36.2 bilioni katika muhula wake wa kwanza na Sh49.1 bilioni katika muhula wa pili.
Pia imebainika kuwa Urais una historia ya kuajiri washauri wengi, ambapo Kenyatta alitumia Sh4.8 bilioni kwa washauri katika kipindi cha miaka 10, huku Ruto akitumia Sh2.9 bilioni kufikia sasa.
Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed alisema ofisi za Rais na Naibu Rais ni ofisi za kikatiba, zikiwa na majukumu, miundo na ufadhili uliobainishwa wazi katika Katiba pamoja na sheria husika.
Vivyo hivyo, majukumu ya Afisi ya Utendaji ya Rais, ofisi ya Naibu Rais, ofisi ya Mkuu wa Mawaziri na Masuala ya Baraza la Mawaziri na idara mbalimbali za serikali chini ya Urais yamefafanuliwa kupitia nyaraka rasmi za kiutendaji na mifumo ya serikali iliyoidhinishwa.
Ni muhimu kusisitiza kwamba matumizi yote ya ofisi hizi, iwe ni ya kawaida au ya maendeleo, huidhinishwa kila mwaka na Bunge kwa mujibu wa mfumo wa kifedha wa kikatiba wa taifa.
Mchakato huu huhusisha uchunguzi wa kina wa majukumu ya ofisi, idadi ya wafanyakazi, mishahara na matumizi ya uendeshaji na kamati husika za Bunge kabla ya kuidhinishwa.
Muundo rasmi wa watumishi, ikiwemo idadi ya wafanyakazi na washauri pamoja na majukumu yao, umeorodheshwa katika rekodi rasmi za utumishi wa umma na unakitwa katika makadirio ya bajeti yanayowasilishwa na kupitishwa na Bunge.
Kuhusu matumizi ya kawaida kama mishahara na gharama za uendeshaji, maelezo ya kina hutolewa katika makadirio ya bajeti yanayochapishwa kila mwaka.