Tuko sawa na Ruto lakini UDA isitudharau, asema Oburu
Kiongozi wa Chama cha Orange Democratic Movement (ODM) Oburu Oginga jana alisema kuwa mazungumzo yanayopendekezwa kati ya ODM na United Democratic Alliance (UDA) hayako hatarini, akieleza kuwa mazungumzo rasmi bado hayajaanza na hakuna kamati ya mazungumzo iliyoundwa.
Oburu alidokeza kuwa mpango wa uhifadhi wa maeneo ya kisiasa unaopendekezwa utahusu UDA pekee chini ya Rais William Ruto, na hivyo kufungua nafasi kwa vyama vidogo vya muungano wa Kenya Kwanza kuwania nafasi zote za uongozi bila vizuizi nchini.
Alipinga madai kwamba mazungumzo kati ya ODM na UDA yamevunjika, akisisitiza kuwa hakuna hata mazungumzo rasmi yaliyowahi kuanza.
“Hamna mazungumzo yaliyokwama kati ya ODM na UDA. Hatuwezi kusimamisha kitu ambacho hakijaanza. Hata hatujaunda kamati ya mazungumzo, hivyo hakuna jambo la kusitisha,” alisema Oburu.
Kauli yake ilijiri baada ya viongozi wakuu wa ODM, kufuatia mkutano wa kamati kuu ya chama, kutangaza kusitishwa kwa mazungumzo ya muungano ili chama kizingatie kujijenga upya na kuimarisha uungwaji mkono kabla ya uchaguzi ujao.
Hata hivyo, Oburu alifafanua kuwa mazungumzo hayo hayajafikia hatua ya kuanza rasmi.
Mgogoro kuhusu mpango wa kuhifadhi maeneo umetawala mjadala wa kisiasa wiki hii, hasa wakati wa ziara ya Oburu London, Uingereza hali iliyozua mjadala kuhusu uwezekano wa mpasuko ndani ya ODM.
“Nataka kulimaliza suala hili. Hakuna tatizo lolote na kuhifadhi maeneo. Lakini kwa sasa hakuna hiyo. Kama ODM hatuhusiki na vyama ambavyo hatujaingia navyo mazungumzo. Kipaumbele chetu ni UDA,” alisema.
Alisema suala hilo litakuwa miongoni mwa ajenda zitakazojadiliwa watakapoketi na UDA kupitia kamati ya kiufundi itakayotangazwa baadaye.
“Uhifadhi wa maeneo ni mojawapo ya mada tutakazojadili na UDA. Ni baadhi ya ajenda zinazotayarishwa na kamati yetu ya kiufundi,” alisema.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa ODM lazima ilinde ngome zake za kisiasa.
“Wanaosema tusilinde maeneo yetu hawako sahihi. Kama hawataki kulinda viti vyao, waondoke wajiunge na vyama vingine. Hii ni demokrasia,” alisema.
Alisema ODM inaendelea kuwa na nguvu katika maeneo kama Nyanza, Magharibi, Pwani na sehemu za Nairobi, akiongeza kuwa chama hicho hakiko tayari kukabidhi maeneo hayo kwa vyama vingine.
“Hatujajiandaa kukabidhi viti tulivyonavyo kwa chama kingine. Tutashindana kwa nguvu,” alisema.
Hata hivyo, aliwataka viongozi wa ODM wasijiamini kupita kiasi, akisema wote watapitia mchakato wa kura za mchujo.
“Watu wasilale wakidhani viti ni vyao moja kwa moja. Tumefungua mfumo kwa wote wanaotaka kugombea kuanzia MCA hadi urais,” alisema.
Oburu pia alikosoa UDA kwa kile alichokitaja kama dharau dhidi ya ODM, akitaja Spika wa Seneti Amason Kingi na Katibu Mkuu wa UDA Hassan Omar.
“Nimesikitishwa na Spika wangu na Katibu Mkuu wa UDA kwa kudharau ODM,” alisema, akitaka Rais Ruto awaadhibu viongozi hao.
Kuhusu hali ya mafuta nchini, Oburu alikiri hatua za serikali kupunguza VAT ya mafuta kutoka asilimia 16 hadi 8 ni hatua nzuri lakini haitoshi kupunguza makali ya maisha kwa wananchi.
“Nimeambia serikali kuwa wananchi hawajafurahishwa na kupanda kwa bei ya mafuta. Nitazidi kushinikiza ipunguzwe zaidi,” alisema.