Wafanyabiashara wawili kukamatwa kwa kuwalaghai mayatima urithi wao wa thamani ya Sh150m
MAHAKAMA ya Milimani imeamuru polisi wawakamate wafanyabiashara wawili wanaoshtakiwa kwa kuwalaghai mayatima wawili jumba la kifahari lenye thamani ya Sh150milioni miaka saba iliyopita.
Hakimu mwandamizi Geoffrey Onsaringo aliagiza polisi wawakamate Mabw Abdisalan Adan Hussein na John Kigomo Mwaura na kuwafikisha kortini Aprili 27,2026 kujibu mashtaka 18 ya ulaghai na ughushi wa hatimiliki za shamba iliyojengwa jumba hilo.
Adan na Kigomo wameshtakiwa pamoja kwa kula njama za kuwalaghai Sadaff Shokatali Habib na Sabahatt Shokatali Habib mali waliyoachiwa na baba yao marehemu Shokat Ali.
Jumba hilo limejengwa katika ardhi ukubwa hektari 0.117 ya thamani ya Sh 150milioni.
Kiongozi wa mashtaka aliomba korti itoe kibali cha kuwakamata wawili hao kwa vile wamekaidi maagizo mara mbili wafike kortini kujibu mashtaka.
Wakili Paul Macharia anayewakilisha mayatima hao aliomba korti iagize polisi wawashike na kuwafikisha kortini wawili hao.
Akipinga kutolewa kwa kibali cha kuwatia nguvuni wakili Joseph Mbalu Mutava anayemwakilisha Adan amelazwa hospitalini Garissa.
“Naomba kesi hii iahirishwe kwa wiki mbili kuwezesha Adan kupona. Aliugua akiwa safarini kutoka Wajir na akalazwa hospitali moja mjini Garissa,” Bw Mutava ambaye ni jaji aliyestaafu aliambia mahakama.
Bw Mutava alieleza hakimu hana habari zaidi kuhusu jina la hospitali aliyolazwa Adan.
Pia alisema hana rekodi za daktari kubaini anachougua.
Akitoa agizo hakimu alisema hakuna ushahidi Adan kuthibitisha ni mgonjwa.
Alisema Kigomo hajulikani aliko na hakutuma wakili kueleza aliko.
“Hakuna sababu zozote zilizowasilishwa na washtaka za kutofika kortini.Hii mahakama imechukulia wamekaidi agizo wafike kujibu mashtaka. Nakubalia ombi la kiongozi wa mashtaka wakamatwe na polisi wafikishwe kortini,” Bw Onsaringo.
Cheti cha mashtaka kilichowasilishwa na mkurugenzi wa mashtaka ya umma DPP Renson Ingonga kimeorodhesha mashtaka 18 dhidi ya Adan na Kigomo.
Shtaka la kwanza linasema wawili hao walikula njama 2019 kuwalaghai Sabahatt na Sadaff shamba lao la thamani ya Sh150milioni.
Shamba hilo na jumba la kifahari lililojengwa mle ndio urithi wao.