Habari za Kitaifa

Upinzani sasa waahidi bonge la maandamano ya kupinga ‘utawala mbaya’

Na PIUS MAUNDU April 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKENYA wametakiwa kujiandaa kwa wimbi jipya la maandamano kuanzia Juni 25, viongozi wa upinzani Kalonzo Musyoka na Rigathi Gachagua wamesema, wakisisitiza kuwa hatua hiyo inalenga kupinga kile wanachokiita “utawala mbaya” wa Rais William Ruto.

Viongozi hao waliokuwa wakihutubia mikutano ya hadhara katika Kaunti ya Kitui walisema maandamano hayo yatakuwa makubwa zaidi na yatadumu zaidi ya yale ya awali, wakiyaita “Maandamano ambayo hayajawahi kushuhudiwa.”

Walitumia ziara hiyo pia kupongeza vijana walioandamana kupinga kupanda kwa gharama ya maisha, hasa ongezeko la bei ya mafuta, wakisisitiza kuwa hawakuhusika kuandaa maandamano hayo.

“Tunapanga maandamano makubwa zaidi Juni 25 kuwakumbuka vijana waliouawa na polisi kwa kupinga serikali,” alisema Musyoka katika eneo la Katutu, akidai kuwa serikali imeshindwa kushughulikia changamoto za kiuchumi zinazowakumba wananchi.

Musyoka alisema kupanda kwa bei ya mafuta kumesababisha mfumko wa gharama ya maisha, akiongeza kuwa sera za serikali hazijafanikiwa kuleta nafuu kwa wananchi.

Alitaja pia hali ya uchumi kuwa “iliyodhoofika,” akiwataka Wakenya kujisajili kwa wingi kupiga kura ili kubadilisha uongozi katika uchaguzi mkuu ujao.

Bw Gachagua alisema upinzani umekuwa ukijipanga kwa muda na kwamba maandamano yajayo hayatahusu tu gharama ya mafuta bali pia masuala ya usalama, utawala bora na mchakato wa uchaguzi.

Alidai kuwepo kwa kile alichokiita “michezo ya kisiasa” ndani ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), akionya kuwa upinzani hautakubali uchaguzi usio wa haki.

“Wale wanaodhani tulikuwa kimya wanakosea. Sisi tuko kwenye maandalizi ya maandamano makubwa zaidi yatakayobadili mwelekeo wa nchi,” alisema Gachagua.

Viongozi wengine wa upinzani kama Eugene Wamalwa na Justin Muturi waliunga kauli hizo, wakilaumu serikali kwa kuongeza ushuru na kushindwa kudhibiti mfumko wa bei.

Muturi alitaka IEBC kushughulikia madai kwamba watu wanajisajili kupigakura mara mbili na pia kuangazia tuhuma dhidi ya viongozi wake wakuu.

Katika mikutano hiyo ya hadhara iliyofanyika Katutu, Tulia, Migwani, Thokoa, Mbondoni na Mwingi, siasa za ndani ya Ukambani pia zilijitokeza wazi.

Gavana Julius Malombe, Seneta Enoch Wambua na Mwakilishi wa Wanawake Irene Kasalu waliungana na viongozi wa upinzani kuimarisha ushawishi wao eneo hilo.

Hata hivyo, mvutano wa kisiasa wa eneo hilo ulionekana kuongezeka baada ya baadhi ya wabunge kuonyesha dalili za kuhama.

Wabunge kama Charles Nguna na Patrick Makau wameonyesha kutoridhika na uongozi wa Wiper, hali inayoashiria mgawanyiko ndani ya chama hicho.

Mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse alikosoa wito wa upinzani wa kuunganisha Ukambani kisiasa, akisema vyama vinavyotaka uongozi wa kitaifa vinapaswa kuwa na uwepo katika nchi nzima.

Alisema chama cha United Democratic Alliance (UDA) kinaendelea kuimarisha mizizi yake mashinani kupitia uchaguzi wa ndani unaoendelea kwa sasa.