Utu wa polisi waibuka wakimsaidia mlemavu aliyekwama kwenye maandamano
Utu wa polisi umejitokeza kwa namna ya kipekee katikati ya maandamano yaliyotikisa mji wa Machakos, ambapo maafisa wa usalama walionekana wakimsaidia mwanaume mlemavu aliyekuwa amenaswa katika vurugu akielekea hospitalini.
Tukio hilo lilishuhudiwa katikati ya taharuki iliyosababisha kufungwa kwa biashara, shule na kusimama kwa shughuli mbalimbali katika mji wa Machakos huku barabara ya Machakos–Kitui ikifungwa na waandamanaji. Polisi walimwagwa maeneo mbalimbali kujaribu kurejesha utulivu na kuwashawishi vijana kufungua njia.
Hali ilianza kuwa tete asubuhi baada ya baadhi ya waendesha bodaboda na madereva wa magari binafsi kusitisha shughuli zao wakitaja mgomo uliotarajiwa kuanza saa nne asubuhi. Hata hivyo, baadhi yao waliendelea kutoa huduma kwa wagonjwa na dharura, wakibeba majeruhi na waliohitaji matibabu.

Katika hali ya kushangaza, afisa mmoja wa polisi alionekana akimwendea mwanaume mlemavu aliyekuwa amekwama katikati ya vurugu hizo na kumsaidia kufika kwenye bodaboda. Afisa huyo alimsaidia kupandishwa kwenye pikipiki hiyo na baadaye kulipia nauli yake ili aharakishe kufikishwa hospitalini.
Wakazi waliokuwa eneo hilo walieleza kuwa tukio hilo lilitoa taswira tofauti ya maafisa wa polisi, ikionyesha huruma na ubinadamu katikati ya mazingira magumu ya usalama.
Hata hivyo, hali katikati ya mji wa Machakos iliendelea kuwa ya wasiwasi baadaye mchana baada ya mapambano makali kati ya polisi na waandamanaji, ambapo gesi ya kutoa machozi na risasi za mpira zilirushwa kuwatawanya vijana waliokuwa wakiziba barabara.

Katika tukio jingine la kusikitisha, afisa wa polisi alikimbizwa hospitalini baada ya mkebe wa gesi ya kutoa machozi kulipuka mkononi mwake alipokuwa akijiandaa kuurusha kuelekea kwa waandamanaji.
Licha ya ghasia hizo, tukio la kumsaidia mlemavu limebaki kuwa alama ya utu katikati ya mvutano mkali uliotawala Machakos.