Guelleh, 78, kuendelea kuiongoza Djibouti baada ya kushinda muhula wa sita
RAIS wa Djibouti, Ismael Omar Guelleh, ameshinda tena uchaguzi kwa kupata asilimia 97.8 ya kura, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali, na hivyo kupata muhula wa sita unaoongeza utawala wake wa zaidi ya miaka 27.
Guelleh mwenye umri wa miaka 78 alitangazwa mshindi baada ya uchaguzi uliofanyika Ijumaa, huku akichapisha ujumbe kwenye mtandao wa X akisema “RÉÉLU”, neno la Kifaransa linalomaanisha “nimechaguliwa tena”.
Ushindi wake haukushangaza wengi, kutokana na uzoefu wake mrefu madarakani na ushawishi mkubwa wa chama chake katika taasisi za kitaifa.
Katika uchaguzi huo, alikabiliana na mgombea mmoja tu wa upinzani, Mohamed Farah Samatar, kutoka chama kidogo kisicho na uwakilishi bungeni.
Vyama viwili vikuu vya upinzani vimekuwa vikisusia uchaguzi tangu mwaka 2016, vikidai kuwa mchakato huo hauwezi kuwa huru wala wa haki.
Taarifa za serikali zinaonyesha kuwa idadi ya wapiga kura waliojitokeza ilikuwa asilimia 80.4.
Katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2021, Guelleh pia alipata zaidi ya asilimia 97 ya kura.
Djibouti ni taifa dogo lenye watu chini ya milioni moja, lakini lina umuhimu mkubwa kimkakati likiwa kwenye Ghuba ya Aden, karibu na lango la Bahari ya Shamu.
Nchi hiyo inahifadhi kambi za kijeshi za mataifa mbalimbali ikiwemo Amerika, China, Ufaransa, Italia na Japan, hali inayolifanya kuwa kitovu muhimu cha usalama na biashara katika eneo la Upembe wa Afrika.
Tangu mwaka 2023, meli kadhaa za kibiashara zilizoharibiwa na mashambulizi ya waasi wa Houthi nchini Yemen zimekuwa zikitia nanga Djibouti, jambo linaloongeza umuhimu wake katika usafirishaji wa kimataifa.
Hata hivyo, mashirika ya haki za binadamu yamekuwa yakikosoa serikali ya Djibouti kwa kukandamiza wapinzani wa kisiasa, wanaharakati na wanahabari. Serikali imekanusha madai hayo na kusisitiza kuwa uchaguzi wake ni wa haki na unaoakisi matakwa ya wananchi.
Licha ya ukosoaji huo, Djibouti imeendelea kudumisha utulivu ikilinganishwa na baadhi ya mataifa mengine ya eneo la Upembe wa Afrika.
Serikali ya Guelleh imewekeza pakubwa katika miundombinu ya bandari, na kuifanya nchi hiyo kuwa lango kuu la biashara kwa taifa jirani la Ethiopia lisilo na bandari.