Kimataifa

Lissu kushtaki kampuni ya simu iliyotoa habari zilizoishia katika jaribio la kumuua

Na REUTERS September 26th, 2024 2 min read

CHAMA kikuu cha upinzani nchini Tanzania kimeitaka kampuni ya mawasiliano ya Tigo kujibu shutuma za mfanyakazi wa zamani kuwa kampuni hiyo ilisaidia serikali kufuatilia alikokuwa kiongozi wa upinzani Tundu Lissu ambaye baadaye alilengwa katika jaribio la kumuua lililoshindikana.

Mfanyakazi wa zamani wa kampuni mlezi ya Tigo, Millicom, aliambia mahakama ya Uingereza mwezi huu kwamba Tigo ilitoa data ya simu ya mkononi kwa serikali iliyoonyesha eneo alikokuwa Tundu Lissu wiki chache kabla ya shambulio hilo.

Gari la Lissu lilifyatuliwa risasi mnamo Septemba 2017 na watu wasiojulikana, kwa mujibu wa stakabadhi za mahakama zilizoonekana na Reuters.

“Nimemfahamisha (wakili) Bob Amsterdam leo kuanza kesi dhidi ya Tigo na serikali ya Tanzania,” Lissu aliambia mkutano wa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa hana imani na mahakama za Tanzania kushughulikia kesi hiyo.

“Tutalazimisha Tigo watuambie walikuwa wanawasiliana na nani. Nani kutoka kwa serikali aliwauliza wanifuatilie saa 24. Itabidi watuambie majina.’

Katika mawasilisho mahakamani mwezi huu, Millicom ilisema ilifahamu mwishoni mwa Agosti au mapema Septemba 2017 kuhusu wasiwasi ‘kuhusu data ya simu ya rununu ya mwanasiasa wa Tanzania kutolewa kwa shirika la serikali’.

Ilisema watu waliohusika walikuwa na nidhamu na mafunzo ya ziada yalitolewa kwa kampuni tanzu za Millicom kuhusu jinsi ya kujibu maombi ya data ya kampuni.

Kampuni hiyo ilikanusha madai katika kesi iliyofunguliwa na aliyekuwa mfanyakazi wake, Michael Clifford, kwamba Clifford alifutwa kazi kwa sababu ya kuibua wasiwasi kuhusu ufuatiliaji wa data za simu ya Lissu.

Kesi hiyo iliripotiwa kwa mara ya kwanza Jumanne na gazeti la Uingereza la The Guardian. Wasemaji wa Millicom na serikali ya Tanzania hawakujibu maombi ya maoni kutoka Reuters Jumatano.

Aliyekuwa rais wa Tanzania wakati huo, John Magufuli alilaani shambulizi dhidi ya Lissu. Hakuna aliyekamatwa au kufunguliwa mashtaka kuhusiana na tukio hilo.

Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye alimrithi Magufuli baada ya kifo chake mwaka 2021, aliahidi kuondoa vikwazo dhidi ya wakosoaji wa serikali vilivyowekwa na Magufuli, lakini mashirika ya kutetea haki za binadamu yanasema serikali imekuwa ikiwalenga wapinzani kabla ya uchaguzi wa unaotarajiwa Desemba. Serikali imekanusha tuhuma hizo.

Mnamo Jumatatu, Lissu alikuwa miongoni mwa viongozi kadhaa wa upinzani waliokamatwa na kuzuiliwa kwa muda na polisi wakijiandaa kuandamana kupinga kile wanachosema ni mauaji na utekaji nyara wa wakosoaji wa serikali.

Imetafsiriwa na Benson Matheka