Magaidi waua waziri wa Ulinzi nchini Mali kwa kulipua makazi yake
BAMAKO, Mali:
WAZIRI wa Ulinzi nchini Mali Sadio Camara aliuawa katika shambulio lililotekelezwa na wanamgambo washirika wa kundi la kigaidi la Al-Qaeda, nyumbani kwake karibu na kambi ya kijeshi iliyoko viungani mwa Bamako, kulingana na taarifa zilizotolewa na vyombo vya habari na jamaa zake wawili, Jumapili.
Shambulio hilo lilitekelezwa na kundi la Jama’at Nasrat al-Islam wal-Muslimin (JNIM) linaloshirikiana na kundi moja la wapiganaji wa Tuareg, katika kile wachanganuzi walitaja kama shambulio kubwa kuwahi kutekelezwa Mali katika miaka ya hivi karibuni.
Jamaa mmoja wa Camara aliambia Reuters kwamba alikuwa ameuawa ilhali mwanahabari wa Mali, ambaye ni shemeji wa waziri huyo wa ulinzi, alichapisha taarifa kuhusu kifo chake katika Facebook.
Hata hivyo, msemaji wa Wizara ya Ulinzi nchini Mali na msemaji wa serikali hawakujibu ombi la Reuters la kuwataka kuzungumzia tukio hilo.
Kulingana na taarifa iliyotolewa na jeshi la Mali, operesheni zinaendelezwa katika sehemu kadhaa nchini humo dhidi ya magaidi na makundi ya waasi.
Mnamo Jumamosi wapiganaji wa kundi la kigaidi la JNIM wakishirikiana na waasi wa Tuareg walitekeleza msururu wa mashambulio nchini Mali katika kile kilichotajwa kama sehemu ya kampeni ya kuangusha serikali ya kijeshi ya nchi hiyo.
Nalo jeshi la Mali lilitangaza kuwa wanajeshi wake walijibu kwa kuwaua “mamia” wa washambuliaji hao huku wakitibua mashambulio mengine yaliyolenga vituo kadhaa ndani na viungani mwa Bamako.
Hata hivyo, makao makuu ya jeshi haikutoa idadi kamili ya wanamgambo wa waliouawa.
Hata hivyo, kwenye taarifa, msemaji wa serikali Issa Ousmane Coulibaly alisema watu 16 walijeruhiwa katika mashambulio yaliyotekelezwa na wanajeshi huku akitoa hakikisho kwamba hali ilikuwa imedhibitiwa katika maeneo yote ambako wanamgambo walitekeleza mashambulio.
Umoja wa Mataifa (UN) ulitoa wito kwa jamii ya kimataifa kuingilia kati kutuliza ghasia na ugaidi katika eneo zima la Sahel kufuatia mashambulio ya Jumamosi.
“Katibu Mkuu amekerwa na ripoti kuhusu mashambulio yaliyotekelezwa katika maeneo kadhaa nchini Mali. Analaani vikali vitendo hivi vya ghasia,” msemaji mmoja wa UN alisema kwenye taarifa aliyochapishwa kwenye mtandao wa kijamii wa X.
Endapo kifo cha Camara kitathibitishwa, kitakuwa pigo kubwa kwa uongozi wa kijeshi nchini Mali, akasema Djenabou Cisse, mmoja wa watafiti katika Wakfu wa Utafiti wa Kimkakati (FRS), inayotafiti kuhusu usalama ukanda wa Afrika Magharibi.
Serikali ya sasa, inayoongozwa na Assimi Goita, iliingia mamlakani baada ya mapinduzi ya 2020 na 2021 na imekuwa ikishirikiana na Urusi huku ikipuuza ushirikiano wa kijeshi kati ya mataifa ya Afrika Magharibi.
Mkakati huo uliendelezwa na Waziri wa Ulinzi, Camara.
“Kama kiongozi mkuu na aliyechangia kuundwa kwa ushirikiano kati ya Mali na Urusi, kuuawa kwake kutakuwa kielelezo kwamba JNIM iko na uwezo wa kulemaza kitovu cha mamlaka ya nchi ya Mali,” Cisse akasema.
Mnamo Jumapili, shirika la habari linasimamiwa na Urusi, Vesti, liliripoti kuwa vikosi maalum vya Urusi nchini humo (Africa Corps) vilipambana na wanamgambo waliokuwa wakishambulia vituo vya serikali ya Mali.
Kulingana na Vesti, wanajeshi wa Urusi walikuwa wakishirikiana na vikosi maalum vya kulinda Rais na wanajeshi, kuzuia uvamizi wa makazi ya rais.
Shirika hilo la habari lilisema baadhi ya wanachama wa “Africa Corps” walijeruhiwa, japo halikutoa maelezo zaidi.
Mashambulio yaliyotokea Mali Jumamosi, ni ishara ya hivi punde kwamba serikali ya nchi hiyo imeshindwa kudumisha usalama licha ya kuahidi kufanya hivyo.