Makosa ya kawaida ya kunyambua vitenzi katika kauli ya kutendesha
KITENZI ni neno ambalo hutumiwa kutoa taarifa kuhusu jambo lililotendeka au lililotendwa.
Vitenzi hubadilika kulingana na wakati vilipotokea.
Vilevile, vitenzi hunyambuliwa kwa kurefusha au kufupisha viishio vyake ili kuonyesha kauli kama vile: kauli ya kutenda, kutendea, kutendeka, kutendesha, kutendeshwa na kutendeana.
Vitenzi katika kauli ya kutendesha aghalabu huchukua viishio vya –sh –a ama –z-a. Kwa hivyo ili mwanafunzi anyambue kitenzi katika kauli ya kutendesha kwa usahihi sharti abainishe ni kiishio gani atatumia.
Mara kwa mara utakumbana na sentensi kama vile:
*Nilipanguza meza baada ya kula kishuka.
*Paka yule alimkimbisha panya.
*Mama yangu aliwatembesha wageni shambani.
*Serikali imepungusha bei ya mafuta.
Katika mifano hii, vitenzi *panguza, kimbisha, tembesha na pungusha vimenyambuliwa visivyofaa.
Mwandishi ana changamoto ya kubainisha viishio –sh-a na –z-a hutumiwa katika neno lipi.
Vilevile, mwandishi anaweza kuwa anakumbwa na changamoto ya kutamka silabi sha na za ipasavyo hasa kutokana na athari za lugha ya kwanza na kuishia kuyaandika maneno hayo kama anavyoyatamka.
Ili kuzisahihisha sentensi hizi tunafaa kusema: Nilipangusa meza baada ya kula kishuka.
Paka yule alimkimbiza panya. Mama yangu aliwatembeza wageni shambani. Serikali imepunguza bei ya mafuta.
Mwanafunzi mwenye changamoto ya kubainisha viishio vya vitenzi anapovinyambua katika kauli ya kutendesha anafaa: kutambua vitenzi vinavyompa changamoyo kunyambua ipasavyo, kufanya mazoezi mengi.
Kisha afanye mazoezi ya kuvitamka vitenzi alivyonyambua kwa usahihi kisha atunge sentensi mbalimbali akitumia vitenzi hivyo.