Habari

Lagat asema vikosi maalum vitaundwa kukabiliana na uhalifu mijini

Na BRIAN OCHARO February 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

IDARA ya Polisi imetangaza mipango ya kuunda vikosi maalum kukabiliana na ongezeko la ukosefu wa usalama jijini Nairobi na katika miji mingine mikubwa huku nchi ikielekea katika kipindi cha kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.

Akizungumza katika makao makuu ya Mamlaka ya Usafiri wa Baharini (KMA) Mombasa wakati wa mkutano uliowaleta pamoja makamanda wakuu wa polisi kutoka kote nchini, Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, Eliud Lagat, alisema kuwa wamepokea maagizo madhubuti ya kukomesha wimbi linaloibuka la uhalifu.

“Hiyo ni sehemu ya mambo tunayojadili katika mkutano huu leo. Makamanda wa polisi wamepewa maagizo makali kushughulikia vitendo hivyo vya uhalifu katika maeneo yao ya uwajibikaji. Tunaunda vikosi maalum kushughulikia hali hii na mtashuhudia msako ukiongezwa kwa kiwango cha juu zaidi,” alisema.

Mkutano huo wa siku tatu umewaleta pamoja makamanda wa polisi nchini, wakurugenzi na makamanda wa vitengo mbalimbali ili kupitia operesheni na mikakati ya kiusalama.

Bw Lagat alisema sehemu ya majadiliano inalenga kusimamia usalama wakati nchi inajiandaa kwa kipindi cha kampeni na uchaguzi utakaofuata.

Pia mkutano huo unajadili masuala ya ustawi wa maafisa wa polisi na namna makamanda wanavyoweza kuwasaidia maafisa walioko mashinani.

“Kimsingi huu ni mkutano wa kimkakati ambao huwa tunafanya, pamoja na masuala mengine tutakayoyajadili kwa faragha,” aliongeza.

Hatua hiyo inajiri wakati ambapo visa vya uhalifu vinaongezeka katika maeneo ya mijini, baadhi yake vikihusishwa na waendesha boda boda na magenge ya kihalifu.

Bw Lagat alisema vyombo vya usalama havitavumilia uhalifu unaojificha ndani ya sekta ya usafiri.

“Tuko wazi kabisa kwamba vitendo vya uhalifu, hasa vinavyoendelezwa na wahuni wanaojificha ndani ya sekta ya boda boda, havitavumiliwa,” alisema.

Alifichua kuwa maafisa wakuu wa usalama wamefanya mazungumzo na Waziri wa Usalama wa Ndani, Bw Kipchumba Murkomen, kufuatia wimbi la hivi karibuni la uhalifu jijini Nairobi na maeneo mengine nchini.

“Pia tuna maagizo ya wazi kutoka kwa Inspekta Jenerali wa Polisi, Douglas Kanja, ya kushughulikia kero la uhalifu kwa uthabiti na kwa mujibu wa sheria. Waendesha boda boda wanapaswa kujua kuwa wako chini ya sheria. Tutamkabili vikali sana yeyote atakayevunja sheria,” alisema.

Katika ukanda wa Pwani, operesheni za pamoja zinaendelea katika kaunti za Kwale, Mombasa na Kilifi ambapo zaidi ya washukiwa kumi wanaohusishwa na magenge ya uhalifu, uporaji wa ardhi na biashara ya dawa za kulevya wamekamatwa.

“Tutaendelea kuweka shinikizo kubwa kwa wahalifu, hasa wanaojihusisha na dawa za kulevya, mashambulizi ya mapanga na aina nyingine za uhalifu wa kupangwa. Shinikizo tayari limeanza na kamanda wa polisi wa kanda amepewa maagizo makali kushughulikia vitendo hivi mara moja,” alisema.

Aliongeza kuwa operesheni zinaendelea pia katika kaunti ya Tana River kufuatia mivutano ya kikabila, huku akiahidi kuwa washukiwa zaidi watakamatwa na kufikishwa mahakamani.

Hivi karibuni, eneo la Pwani limekumbwa na mashambulizi ya makundi yanayojulikana kama panga boys, ambayo yamehusika katika kujeruhi, kuiba na hata kuwaua wakazi.

Vyombo vya usalama vimehusisha kuibuka kwa makundi haya na matumizi ya dawa za kulevya, ukosefu wa ajira na ufadhili wa kisiasa hasa wakati wa kampeni.

“Makundi haya ya kihalifu yatafikia mwisho. Hakuna njia mbili kuhusu hilo. Tumewatambua wafadhili, wanaochochea na kuwalipa vijana kufanya vitendo hivi. Iwe ni mwanasiasa au mwanajamii yeyote, bila kujali wewe ni nani, uko chini ya sheria,” alisema Lagat.

Kuhusu uporaji wa ardhi katika eneo la Pwani, alisisitiza haja ya ushirikiano wa taasisi mbalimbali na kufuata utaratibu wa kisheria.

Aliongeza kuwa mara uchunguzi utakapokamilika na mafaili kuwasilishwa katika hatua inayofuata, hatua stahiki za kisheria zitachukuliwa.

“Tumeainisha maeneo yanayoshuhudia vitendo hivi vya uhalifu na tunaongeza shinikizo kubwa. Itakuwa chungu, lakini ni lazima utaratibu udumishwe,” alisema.

Alionya kuwa wote wanaojihusisha na uhalifu hawana nafasi nchini na kwamba taasisi zote za serikali zitawachukulia hatua wahusika wa mashambulizi ya mapanga, biashara ya dawa za kulevya na pombe haramu kwa mujibu wa sheria.