Majonzi tele kwenye ibada ya kuwaaga wanafunzi 15 waliokufa kwenye mkasa wa moto Utumishi Girls
MACHOZI, majonzi na hali ya kukata tamaa vilitawala ibada ya kuwaaga wanafunzi 15 waliopoteza maisha yao kufuatia moto ulioteketeza bweni la Shule ya Upili ya Utumishi Girls Academy, Gilgil, kaunti ya Nakuru wiki mbili zilizopita.
Mwanafunzi mmoja aliyefariki alizikwa wiki iliyopita katika Kaunti ya Kilifi kwa mujibu wa taratibu za Kiislamu baada ya matokeo ya uchunguzi wa DNA kuthibitisha mwili wake.
Katika ibada hiyo iliyofanyika Uwanja wa Gilgil, viongozi wa kisiasa, wazazi na viongozi wa kidini walitoa wito wa kukomeshwa kwa lawama na badala yake kuanzishwa kwa mazungumzo ya kitaifa ili kutafuta suluhu ya kudumu kuhusu migomo ya wanafunzi, uharibifu wa mali na vifo vinavyoshuhudiwa shuleni.
Mke wa Rais Rachel Ruto, Waziri wa Elimu Julius Ogamba, Gavana wa Nakuru Susan Kihika pamoja na Maseneta Tabitha Karanja na Edwin Sifuna waliongoza waombolezaji kutoa heshima zao kwa wanafunzi hao. Katika ujumbe uliosomwa na Waziri Ogamba, Rais William Ruto alisema serikali itachukua hatua kuhakikisha janga kama hilo halitokei tena katika shule za Kenya. “Kwa familia zilizoathirika, serikali iko pamoja nanyi. Kwa kila mzazi anayempeleka mtoto shuleni kwa matumaini, ninaahidi sitapumzika hadi shule zetu ziwe mahali salama,” alisema Rais.
Bi Ruto alisema taifa linaomboleza pamoja na familia zilizoathirika huku akiwapa pole manusura wanaoendelea kupona. Wakati huo huo, wanafunzi tisa bado wanazuiliwa na polisi wakishukiwa kumwaga mafuta ya taa kwenye godoro na kuwasha moto usiku wa Mei 27, tukio lililosababisha vifo vya wanafunzi 16 na majeraha kwa wengine 79.
Wiki iliyopita, wanafunzi saba waliokuwa wakipokea matibabu katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta waliruhusiwa kwenda nyumbani, ingawa watatu wao wataendelea kutumia viti vya magurudumu kwa muda wanapoendelea kupona.
Miili ya wanafunzi hao iliwasili uwanjani ndani ya magari 15 ya kubebea maiti huku maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai, Huduma ya Vijana kwa Taifa na Shirika la Msalaba Mwekundu wakisimamia shughuli hiyo.
Majeneza meupe yaliyopambwa kwa maua yalipangwa mbele ya waombolezaji huku wazazi wakishikilia picha za watoto wao, wengi wakishindwa kujizuia na kububujikwa na machozi. Kutokana na majeraha makubwa ya moto, miili haikuonyeshwa hadharani.
Gavana Susan Kihika alisema zaidi ya shule 200 zimekumbwa na migomo na vurugu katika wiki tatu zilizopita, hali iliyowaathiri zaidi ya wanafunzi 4,000.
“Hatuwezi kupuuza mazingira ambayo watoto wetu wanakulia. Wanatuangalia, wanatusikiliza na kuiga mienendo yetu. Wakiona watu wazima wakitatua migogoro kwa vurugu, nao huamini hiyo ndiyo njia sahihi,” alisema.
Maseneta Tabitha Karanja na Edwin Sifuna pamoja na Mbunge Mwakilishi wa Wanawake wa Kiambu Ann Wanjiku Muratha walitaka mazungumzo ya kitaifa kuhusu nidhamu shuleni na usimamizi wa majanga.Sifuna alisema mkasa huo unaonyesha kushindwa kwa viongozi kuhakikisha hatua za usalama zinawekwa shuleni. Kwa upande wake, Waziri Ogamba alisema kuna haja ya kutathmini namna jamii na serikali zinavyowalea watoto.
Aliongeza kuwa shinikizo la maisha, matatizo ya kiakili pamoja na matumizi ya dawa za kulevya yamechangia kuongezeka kwa vurugu shuleni na kwamba, serikali itaunda jopo la wadau mbalimbali kutafuta suluhu ya kudumu.
Mchungaji John Kivuva wa Kanisa la African Inland Church aliwahimiza wanafunzi walionusurika kujifunza kutokana na tukio hilo na kutochezea moto, akisema maisha ni ya thamani kubwa.
Nahodha wa shule hiyo, Abigael Wanjiku, aliwakumbuka wenzake kama dada, marafiki na washirika waliokuwa na ndoto kubwa za maisha.
Naye Grace Wacheke aliyewakilisha familia zilizoathirika aliwasihi manusura kutafuta msaada wanapohisi kulemewa na huzuni, akisema majeraha ya tukio hilo ni ya kimwili na pia ya kisaikolojia.
Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Langat, ambaye pia ni mlezi wa shule hiyo, alisema wanafunzi hao walikuwa mabinti wenye ndoto na matumaini makubwa, akisisitiza kuwa uchunguzi wa kina lazima ufanywe ili ukweli ujulikane na kuhakikisha janga kama hilo halitokei tena.