Habari

Mekatilili wa Menza kujengewa sanamu ya kumbukumbu Shakahola

Na ANTHONY KITIMO May 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZEE wa Chama cha Utamaduni cha Wilaya ya Malindi (MADCA) pamoja na serikali ya Kaunti ya Kilifi wametangaza mipango ya kumuenzi shujaa wa uhuru, marehemu Mekatilili wa Menza kupitia ujenzi wa sanamu katika eneo la Shakahola.

Kulingana nao, Mekatilili alinza mapambano ya uhuru katika eneo hilo la Shakahola miongo ya kale kabla Kenya kupata uhuru.

Hospitali mpya ya kina mama ya Malindi pia inatarajiwa kutajwa jina la kiongozi huyo wa zamani wa uhuru.

Tangazo hilo linafuatia mashauriano Kati ya MADCA wakiongozwa na Mzee Joseph Karisa Mwarandu na gavana Gideon Mung’aro.

“Tumekubaliana kujenga sanamu kubwa eneo la Shakahola, eneo la kihistoria ambapo Mekatilili alianza mapambano yake dhidi ya ukandamizaji wa wakoloni,” alisema Bw Mwarandu.

Gavana Mung’aro alisema sanamu hiyo itakuwa kumbukumbu ya kudumu ya ujasiri wake na ukumbusho wa harakati za jamii za kujitawala.

Aidha, Hospitali mpya ya Wanawake ya Muyeye iliyokamilika mjini Malindi itapewa jina la Hospitali ya Mekatilili, ikiwa maalum kwa huduma za afya ya uzazi na kujifungua salama.

Gavana huyo alibainisha kuwa hatua hiyo sio tu ya kumuenzi shujaa huyo bali pia inaimarisha huduma za afya kwa akina mama kote Kaunti ya Kilifi.

Bw Mung’aro pia alifichua kuwa barabara kadhaa zinazojengwa zitapewa majina ya mashujaa wa eneo hilo na wa Pwani ili kuhakikisha urithi wao unahifadhiwa kwa vizazi vijavyo.

“Ni lazima tusherehekee historia yetu kwa kuiweka ndani ya miundombinu na taasisi zetu,” alisema.

Mekatilili wa Menza, anayeheshimika kama mmoja wa wapiganiaji wa kwanza wa uhuru wanawake nchini Kenya, aliwaongoza Wagiriama kupinga utawala wa kikoloni wa Waingereza mwanzoni mwa karne ya 20.

Ujasiri na uongozi wake ulimfanya kuwa ishara ya uthabiti na uwezeshaji, hasa kwa wanawake katika harakati za kutafuta haki.

Tangazo la gavana huyo linaonyesha juhudi pana za kuunganisha urithi wa kitamaduni katika miradi ya maendeleo, huku ikiimarisha utambulisho wa Kilifi na kukuza fahari ya mashujaa wake wa kihistoria.

Kwingineko, viongozi na maafisa wa usalama katika Kaunti ya Kilifi, wamehimiza wakazi kushirikiana nao ili kukabili magenge ya uhalifu.

Hayo yalisemwa baada ya mkutano ulioleta pamoja maafisa wa usalama wakiongozwa na Kamanda wa polisi ukanda wa Pwani, Bw Ali Nuno, na viongozi wa kaunti wakiongozwa na Gavana Mung’aro.

Waliahidi kuimarisha doria, kuboresha ushirikiano, na kuongeza ushiriki wa jamii ili kurejesha usalama.

Katika siku za hivi majuzi, wafanyabiashara wameripoti visa vya uvamizi wa madukani maeneo mbalimbali ya Kilifi, huku wavuvi katika eneo la Mayungu, wakisema wanahofia magenge ya Mawozawoza yanayowalenga wanaporejea kutoka baharini na kuwapora samaki wao.

“Usalama wenu ni jukumu langu la kwanza. Lakini tunahitaji kila mmoja kutekeleza wajibu wake,’ alisema Gavana Mung’aro.

Bw Nuno naye alisema watashirikiana na wananchi kupata habari muhimu na kuchukulia washukiwa hatua za kisheria.

‘Wakazi wanajua wanaotekeleza maovu katika miji yetu. Tutatumia habari ambazo mtawasilisha kwetu ili kuhakikisha visa hivi vinakomeshwa,’ alisema Bw Nuno.