Taharuki juhudi za kufuta wilaya za watu weusi Amerika zikianza
TAHARUKI kuhusu uchaguzi imegubika jimbo la Louisiana kutokana na uamuzi uliotolewa wiki iliyopita na Mahakama ya Upeo uliobuni kipengee muhimu cha sheria kuhusu haki za umma.
Uamuzi huo uliwapa wabunge wa Republicans fursa ya kuchora ramani mpya inayofuta wilaya moja au mbili za Democratic katika jimbo hilo zenye idadi kubwa ya watu weusi.
Wapigakura wenye ngozi ya rangi nyeusi wanajumuisha thuluthi moja ya wapigakura jimboni Louisiana na kwa kawaida huunga mkono chama cha Democratic. Republicans tayari inadhibiti wilaya nyingine nne.
Siku moja baada ya uamuzi wa Korti ya Upeo, Gavana Jeff Landry aliahirisha chaguzi za vyama kuhusu ubunge nchini zilizopangiwa kufanyika Mei 16, hata ingawa maelfu ya madebe ya kura yalikuwa yamewasilishwa.
Wapigakura waliowasili sehemu za upigaji kura mapema wiki hii walikumbana na ilani zilizobandikwa kwenye milango zikitangaza kuwa chaguzi za ubunge zimefutiliwa mbali, huku vinyang’anyiro vingine vikiendelea.
Bado haijabainika kitakachofanyika kwa kura zilizokwisha kupigwa na ni lini chaguzi za vyama zitaratibiwa upya.
Maswali kuhusu mchakato huo yangesuluhishwa na katibu wa jimbo Louisiana, mwenyekiti wa kamati ya Republican, Caleb Kleinpeter alieleza wanahabari baada ya kusikizwa kwa kesi hiyo.
“Ukweli wa suala hili ni kuwa Mahakama ya Upeo ilikuja na ikasema ramani hizo ni kinyume cha katiba,” alisema. Kwa hivyo “tunasonga mbele na uchoraji wa ramani mpya”.
Akiwa mtoto, Leona Tate alikuwa moja kati ya wanafunzi weusi wa kwanza almaarufu “Wanne wa New Orleans” kujumuika katika shule ya umma mashinani Kusini, wakistahimili ubaguzi wa rangi na vitisho vya kuuawa, Jeshi la Nchi lilipowasindikiza darasani.
Ijumaa, zaidi ya miongo sita baadaye, Tate aliwaeleza wabunge wa Republican kwamba pendekezo lao la kuvunjilia mbali wilaya moja au zaidi zenye idadi kubwa ya watu weusi lilifufua kumbukumbu hizo za kutisha.
“Nataka mwelewe inavyohisi kusimama hapa, kutembea katikati ya halaiki ya watu kama mtoto, na sasa kuwatazama maafisa waliochaguliwa wakifanya jambo lile lile umma ulijaribu kufanya – tofauti tu ikiwa suti bora na mchakato wa bunge,” alieleza kikao cha kamati ya seneti katika jiji kuu la Baton Rouge.
Kwa zaidi ya saa nane, wabunge weusi wa Congress, mapasta, wanaharakati na wapigakura walitoa ushahidi ambao wakati mwingine ulivutia hisia za hasira na za kisiri.
Nje ya chumba cha kusikiza kesi, umati uliwashangilia kuendelea.
“Acha azungumze!” Waliimba wakati mmoja baada ya Kleinpeter kuzima kipaaza sauti cha mbunge mwenzake wa Democratic katikati ya majibizano makali.
Mike McClanahan, rais wa shirika kubwa zaidi la kutetea haki za kibinadamu nchini kwa jina NAACP, Louisiana, alizuiwa kimabavu kuingia chumba hicho na ulinzi wa seneti.
Louisiana ndiyo ya hivi majuzi kwenye mzozo kitaifa unaohusu mchakato wa kuunda upya wilaya ulioanzia Texas mwaka jana na kushika kasi wiki hii kote Kusini ikiwemo Tennessee, Alabama na South Carolina, ambapo wana Republicans walijibu maamuzi ya korti ya upeo kwa kuanzisha juhudi sawia za kuangamiza wilaya zinazosheheni idadi kubwa ya weusi.
Wanademocrats wameanzisha juhudi zao binafsi za kuunda upya wilaya, lakini azma yao ilipata pigo kuu Ijumaa wakati Mahakama ya Upeo Virginia ilipotupilia mbali ramani mpya iliyopitishwa na wapigakura ambayo huenda ingebadilisha viti vinne vya Republican.
Kilichokuwa kinyang’anyiro chenye usawa cha kuchora upya ramani za bunge sasa kimegeuka kwa kishindo kuegemea Republican kabla ya uchaguzi wa katikati ya muhula November, ambapo itatetea idadi iliyobanwa ya waliowengi bungeni.