Habari

Matiang’i asema yeye ndiye dawa ya Ruto

Na JUSTUS OCHIENG February 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

NAIBU Kiongozi wa Jubilee Dkt Fred Matiang’i ambaye ni mmoja wa vinara wa muungano wa upinzani anaahidi kuboresha uongozi iwapo atashinda urais katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Akishutumu uongozi wa Rais William Ruto kwa utawala mbaya, Dkt Matiangi alisema utawla wake hautavumilia ufisadi na uzembe.
Alisema hayo katika mahojiano ya kipekee ambapo alionya ni lazima muungano wa upinzani uwe makini kuteua mgombea urais wa pamoja.
Alisema chama cha Jubilee kinachoongozwa na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta kinashinikiza kuwepo kwa mfumo wa kisayansi wa kumpata mgombea mmoja wa urais wa Muungano wa Upinzani, kikionya kuwa makubaliano ya siri ya viongozi wachache yanaweza kuvunja muungano huo kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Tayari, kikao muhimu kilichokuwa kianze leo katika mji wa Naivasha kimeahirishwa hadi wiki ijayo, huku taarifa zikionyesha kuwepo kwa mvutano kuhusu njia bora ya kumteua mgombea wa pamoja wa urais.
Katika mahojiano maalum, alisema mbinu itakayotumika kumchagua mgombea wa pamoja itaamua hatima ya muungano wa upinzani au kumpa Rais William Ruto njia rahisi ya kurejea mamlakani kwa muhula wa pili.
Katika mahojiano hayo, Dkt Fred Matiang’i alirejelea mara kwa mara hoja moja kuu: uongozi.
“Tatizo la Kenya ni uongozi, basi,” alisema. “Tuna uongozi wa kujinufaisha binafsi unaojikita katika uporaji wa rasilmali za nchi na kujaza mifuko yao.”
Aliahidi kupambana na ufisadi “kana kwamba maisha yangu yanategemea hilo,” akirejelea kipindi chake serikalini ambapo anasema alitekeleza mageuzi ndani ya mifumo ya kisheria iliyokuwepo na kutetea maamuzi yake mahakamani kwa mafanikio.
Pia alitoa wito wa ajira katika utumishi wa umma kuzingatia misingi ya uwezo na sifa, na kukomesha kile alichokitaja kuwa uteuzi wa upendeleo wa kisiasa.
“Vijana hawatuombi tuwapikie. Wanatuomba tufanye kazi yetu ili fursa zipatikane,” alisema.
Huku viongozi wa upinzani wakipanga kikao chao cha mashauriano, matarajio ni kwamba wataweka wazi mwelekeo wao wa sera pamoja na ramani ya uteuzi wa mgombea.
Dkt Matiang’i alitaja kikao hicho kama fursa ya kutafakari na kuoanisha vipaumbele. “Tutajadili namna ya kusonga mbele, namna ya kushirikisha Wakenya na vipaumbele vyetu ,” alisema.
Wadau wa karibu wanasema kikao hicho kinaweza ama kuimarisha njia iliyo wazi kuelekea umojaau kufichua tofauti ambazo hazijatatuliwa.
Iwapo mtazamo wa Dkt Matiang’i utakubalika, muungano unaweza kupitisha mfumo wa uteuzi unaotegemea takwimu na ushahidi, unaolenga kuwapa wafuasi wa maeneo na vyama mbalimbali imani. Usipokubalika, hatari ya mgawanyiko itakuwa kubwa.
Dkt Matiang’i alisisitiza kuwa mchakato huo unapaswa kuwa wa kisayansi, wazi, shirikishi na wenye kuaminika. Alionya kuwa uamuzi wa kufanyika kwa makubaliano ya “vyumba vya siri” kati ya watu wachache hautadumu mara utakapowekwa wazi kwa umma.
“Hauwezi kushinikiza vyama, viongozi na wapigakura hadi uamuzi fulani bila kuwahusisha kikamilifu. Matokeo yake yatakuwa mabaya,” alisema.
Kauli yake inakuja huku upinzani ukijaribu kuunganisha vyama na wanasiasa wenye ushawishi, akiwemo aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, kiongozi wa PLP Martha Karua, kiongozi wa DAP-K Eugene Wamalwa na kiongozi wa DP Justin Muturi—wote wakitajwa kuwa na nia ya kupeperusha bendera ya muungano huo.
Dkt Matiang’i alisema iwapo wagombea wanne au watano watashindania tiketi hiyo, basi wale watakaoshindwa lazima waweze kurejea kwa wafuasi wao na kueleza kwa hoja na ushahidi kwa nini hawakushinda. Bila mchakato wa haki na unaoaminika, alionya, hali hiyo itageuka kuwa ushindani wa mshindi kuchukua yote, huku waliobaki wakikosa hamasa ya kumuunga mkono mshindi.
Alirejelea historia ya siasa za miungano nchini, akitaja mfano wa uchaguzi wa 2007 ambapo Kalonzo Musyoka alijiondoa katika kundi la ODM Pentagon lililomjumuisha marehemu Raila Odinga na kugombea urais kivyake dhidi ya Raila na Mwai Kibaki. Hatua hiyo ilisababisha mgawanyiko mkubwa ambao uliathiri matokeo ya uchaguzi huo.
Aidha, alikumbusha kuwa hata mwaka 2022 kulizuka mvutano baada ya uteuzi wa mgombea mwenza katika muungano wa Azimio, hali iliyoonyesha changamoto za kufikia makubaliano ya haki ndani ya miungano.
Kwa mujibu wa Dkt Matiang’i, kamati ya kiufundi inayoongozwa na aliyekuwa Waziri wa Kilimo Kipruto Arap Kirwa imepewa jukumu la kuchunguza mfumo bora wa kumpata mgombea wa pamoja. Hata hivyo, alisisitiza kuwa mapendekezo yake lazima yaweze kutetewa mbele ya umma.
“Ikiwa ni kura za maoni, basi ziwe za kisayansi na zifuate viwango vinavyokubalika. Haiwezi kuwa mimi na wewe na watu wawili wengine tunaketi chumbani na kuamua. Uamuzi huo utaporomoka siku ileile utatangazwa,” alionya.
Alisema iwapo mchakato hautazingatia heshima na uadilifu, utamfaidi moja kwa moja Rais Ruto, kwa kuwa upinzani uliogawanyika ndio mtaji mkubwa wa kisiasa kwa aliye mamlakani.
Kuhusu madai ya kuwepo kwa mvutano kati yake na Bw Gachagua, Dkt Matiang’i alikanusha akisema hana uhasama na yeyote. “Sina ugomvi na mtu yeyote. Mimi ni Fred tu ninayetaka kuleta matokeo,” alisema, akijitaja kama mtaalamu asiye na mizigo ya kisiasa.