Habari

2027: ODM pabaya, vyama vya UDA, Wiper vikipenya eneo la Pwani

Na ANTHONY KITIMO April 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ENEO la Pwani ambalo kwa muda limekuwa ngome ya chama cha ODM sasa linaonekana kuponyoka ‘mtego’ was chama cha chungwa ambacho kwa sasa kinakumbwa na mgogoro ndani ya uongozi.
Vyama visivyo kuwa na ushawishi katika eneo hilo kama vile Wiper na UDA vinaonekana vikizidi kujikakamua na kuongeza wanachama jambo ambalo linaongeza wasiwasi kwa viongozi wa ODM.
Siku ya Jumamosi, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka aliidhinisha mbunge wa Nyali Mohammed Ali na mwenzake wa Wundanyi Danson Mwashako kama wagombeaji wa ugavana mwaka ujao kupitia chama cha wiper Mombasa na Taita-Taveta mtawaalia.
Kuteuliwa kwa viongozi hao linaongeza ushindani kwa Kaunti ambazo miaka ya nyuma ilikuwa na wafuasi wengi wa chama cha ODM.
Wakati wa kupendekezwa kwako, Bw Ali alisema mwaka ujao utakuwa mwanzo mpya kwa wakazi wa Mombasa na akaahidi kuwa hataruhusu Mombasa kuzama kwa uongozi duni.
“Hatuwezi kukaa tu na kutazama Mombasa ikigeuka kuwa makumbusho ya ndoto zilizovunjika. Lazima tuiamini Mombasa si kwa ilivyo sasa, bali kwa jinsi inavyoweza kuwa na tunaendelea kushirikiana na kusikiliza sauti ya wananchi inayotaka mabadiliko!” alisema Ali.
Kauli hiyo inaonekana kuwa hatua muhimu katika mkakati wa upinzani kuimarisha uungwaji mkono katika siasa za pwani.
Bw Kalonzo alisema upinzani ulikubaliana kuunga mkono Bw Ali na Bw Mwashako baada ya mashauriano yaliyohusisha viongozi wengine wa muungano wa United Opposition. Alisema uamuzi huo unalenga kuongeza nafasi zao katika kaunti ambayo bado ina ushindani mkubwa wa kisiasa.
“Tumeungana tumfanye na tusaidie nyinyi watu wa Pwani. Hawa viongozi wa Nyali na Wundanyi hawana madoa yoyote ya wizi hivyo tunawaunga mkono kwa dhati,” alisema Bw Kalonzo.
Bw Kalonzo pia alirejelea mashindano ya kisiasa yaliyopita Mombasa, akitaja mivutano na mazungumzo yaliyounda siasa za upinzani katika eneo hilo. Alikumbuka kipindi cha mwaka 2022 ambapo viongozi, akiwemo aliyekuwa kinara wa ODM Raila Odinga, walifanya kampeni kubwa kaunti hiyo kumuunga mkono gavana wa sasa Abdulswamad Sheriff Nassir.
Bw Mwashako kwa upande wake alisema kazi take aliyofanya kama mbunge kwa miaka 10 ndiyo inamtetea kwenda kiti cha Ugavana Taita-Taveta.
Vyama vingine pia vimeendeleza kampeni kutwaa viti vikuu Pwani.
Hapo UDA na ODM wote wanaunga mkono Raisi William Ruto kwa awamu yake ya pili kwa sasa, viongozi wa vyama hivyo wametofautiana kuhusu wagombeaje wa viti vingine.
UDA tayari imeweka vigogo katika ngome zilizomilikiwa na ODM kama vile Kilifi, Mombasa na Tana River Jambo ambalo halifurahiwi na wanachama wa ODM
Katika Kaunti ya Kilifi, Bi Aisha Jumwa amejitosa uwanjani kwa tiketi ya UDA kumpinga Gavana Gideon Mung’aro.
Katika Kaunti ya Mombasa, katibu wa chama cha UDA Hasan Omar ameonekana akinowa makali kukabiliana na Gavana Abdulswamad Nassir huku Hussein Dhado wa UDA akijipanga kumrithi Gavana wa Tana River Dhadho Godhana ambaye anamaliza mihula yake miwili.
Licha ya hayo, Waziri wa Madini na Uchumi Baharini Hassan Joho ameahidi kuendeleza kampeni kali kuhakikisha ODM inabaki na wanachama wengi.
Siku ya Jumapili, vigogo wa ODM walikutana Malindi na wabunge zaidi ya 20 ambapo waliahidi kuungana na kuendeleza uongozi wa chama hicho