Habari

Mwanakemia apata DNA ya Matara kwenye kondomu chumba alikouawa Starlet Wahu

Na RICHARD MUNGUTI February 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MTAALAMU wa maabara ya Serikali alieleza mahakama kuu Jumanne, Februari 10, 2026 kwamba sampuli ya damu iliyokuwa kwenye kisu na taulo zilizotolewa kwenye chumba cha kulala alikouliwa Starlet Wahu ilikuwa yake.

Bi Emilly Okworo alisema alitumia utaalamu wa kulinganisha chembechembe za DNA kwenye vifaa alivyopelekewa na polisi na ile damu iliyotolewa kwenye mwili wa Starlet.

“Nilipolinganisha DNA kwenye damu ya Starlet na ile iliyokuwa kwenye vifaa — kisu na taulo — zililingana na nikafikia uamuzi ilikuwa damu ya binadamu. Damu hiyo ilikuwa ya Starlet,” akasema Bi Okworo.

Mwanakemia huyo wa Serikali alisema vile vile alikagua kiutaalamu shahawa zilizokutwa ndani ya kondomu iliyookotwa katika chumba alikouliwa Starlet.

Alisema shahawa hizo zilikuwa za mwanamuziki, John Matara anayeshtakiwa kwa mauaji ya Starlet Wahu.

Starlet alikuwa dadaye mdogo wa Pasta Victor Kanyari.

Bi Okworo aliyeongozwa kutoa ushahidi wake na kiongozi wa mashtaka Bi Dela Wilbey alisema alifanyia sampuli hizo utafiti wa hali ya juu kabla ya kutoa ripoti yake kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma Renson Ingonga.

Mwanakemia huyo alisema hana tashwishi na ripoti hiyo yake hata!

“Niko na uhakika mia kwa mia kwamba sampuli za damu nilizopima zilikuwa za Starlet,” akasema Bi Okworo.

Alisema kulikuwa na damu ya mtu watatu ambaye hakufichuliwa jina lake.

Lakini mawakili Samuel Ayorsa na James Mochere wanaomtetea Matara waliambia mahakama kwamba kulikuwa na sampuli nyingine ya damu ya mtu ambaye hajulikani.

Mawakili hao walisema pia Matara alijeruhiwa wakati wa kizaazaa hiki na hata damu yake iliguduliwa kwenye taulo iliyokutwa ndani ya chumba cha Air BnB.

Mahakama ilionyeshwa kisu kilichotumika kumchinja Starlet.

Matara ameshtakiwa kumuua kinyama Starlet.

Alinyimwa dhamana na mahakama kuu.

Anazuiliwa katika gereza kuu la Kamiti.