Mkosoaji mkuu wa serikali Afrika Kusini Julius Malema atupwa jela kwa kumiliki bunduki
KUGOMPO CITY, AFRIKA KUSINI:
MWANASIASA wa upinzani Afrika Kusini Julius Malema jana alifungwa miaka mitano gerezani kwa kumiliki bunduki kinyume cha sheria na kufytua risasi hadharani.
Malema alishtakiwa mwaka jana kwa kuwa na bunduki bila leseni na kuitumia hadharani mnamo 2018.
Alijitetea kuwa alitumia bunduki hiyo isiyo yake kusisimua wafuasi wa chama chake wakati walikuwa wakiadhimisha miaka mitano ya uwepo wa chama hicho.
Baada ya uamuzi huo, mawakili wake walikata rufaa ili asifungwe gerezani.
Akiwa amesimama kortini akiwa amevalia suti nyeusi na tai nyekundu, Malema hakuonekana kutishwa na hukumu hiyo hata wakati Hakimu wa Mahakama ya East London Twanet Olivier alipokuwa akisoma uamuzi wake.
Malema, 45 ni mwanasiasa wa upinzani ambaye amekuwa akikosoa mno utawala wa Rais Cyril Ramaphosa na anashabikiwa sana na watu weusi Afrika Kusini.
Mwanasiasa huyo anaongoza chama cha EFF na mnamo Jumatano alikanusha mashtaka dhidi yake Chama chake cha EFF ndicho cha nne kwa ukubwa katika siasa za Afrika Kusini.
Angefungwa kwa kipindi kinachozidi miaka 12 basi Malema hangeendelea kuhudumu kama mbunge kulingana na sheria za Afrika Kusini.
Hilo lingekuwa pigo kwa vijana wa Afrika Kusini ambao ni wafuasi wa Malema na wamekuwa wakilalamika kwamba wamebaguliwa tangu taifa hilo lijinyakulie uhuru mnamo 1994.
Kortini, kiongozi wa mashtaka alisema kuwa itakuwa mfano mbaya iwapo Malema atawaachiliwa huru bila kuhukumiwa kifungo.
“Mshtakiwa ni mwanasiasa ambaye ana ufuasi mkubwa na anashabikiwa na vijana wengi ambao wanaweza kuiga tabia hii yake,” akasema Kiongozi wa mashtaka Joel Ceasar.
“Yeye ni mbunge, mtunga sheria lakini anavuruga sheria hiyo hiyo,” akaongeza.
Mawakili wa Malema nao walimtetea wakisema hakulenga kutumia bunduki hiyo kuua na alikuwa tu akifanya hivyo kusherehekea. Mawakili hao wanataka Malema asifungwe na apigwe tu faini.