Habari

ODM sasa yamkalia Ruto ngumu kuhusu 2027, yataja matakwa 8

Na MOSES NYAMORI August 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha ODM kimeweka matakwa manane mbele ya Rais William Ruto kabla ya uchaguzi wa 2027, huku viongozi wa chama hicho wakitarajiwa kuyajadili katika mkutano wa siku tatu wa serikali jumuishi unaoanza Naivasha leo Jumapili.
Mkutano huo unawakutanisha magavana, manaibu wao na wabunge wa ODM, UDA na vyama vingine vinavyounga mkono serikali jumuishi.
Ingawa mkutano huo umeelezwa kuwa wa kuimarisha uhusiano na kujenga mwafaka, ODM inataka serikali itekeleze makubaliano yaliyofikiwa kabla ya chama hicho kuendelea kushirikiana na UDA kuelekea uchaguzi wa 2027.
ODM inataka utekelezaji wa ajenda ya vipengele 10 iliyokuwa msingi wa makubaliano ya kisiasa kati ya Rais Ruto na marehemu aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga.
Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga alisema viongozi watapitia hatua zlizopigwa katika kutekeleza makubaliano hayo.
Ajenda hiyo inahusisha masuala yaliyokubaliwa na pande hizo mbili wakati wa mazungumzo yaliyolenga kupunguza mvutano wa kisiasa nchini.
ODM pia inataka serikali kutoa mwelekeo kuhusu miswada iliyotokana na Kamati ya Mdahalo wa Kitaifa (Nadco).
Baadhi ya mapendekezo ya Nadco yalihusu kuanzishwa kwa afisi ya Kiongozi Rasmi wa Upinzani na Waziri Mkuu.
Chama hicho kinataka kujua hatua ambayo serikali imechukua kutekeleza mapendekezo hayo.
ODM inataka hatua zaidi kuchukuliwa kuhusu fidia kwa waathiriwa wa ukatili wa polisi.
Bi Wanga alisema suala hilo litakuwa miongoni mwa mambo yatakayojadiliwa katika mkutano huo.
Hii ni mojawapo ya masuala ambayo chama hicho kinataka serikali ishughulikie kama sehemu ya makubaliano yaliyofikiwa.
ODM pia inataka kuwe na uwazi kuhusu mustakabali wa ushirikiano wake na UDA kuelekea uchaguzi wa 2027.
Chama hicho kinataka kujua jinsi ushirikiano huo utakavyofanya kazi na nafasi ya kila chama katika maandalizi ya uchaguzi.
Huku uchaguzi ukikaribia, viongozi wa vyama hivyo wameanza kushindana kuhusu maeneo ya kisiasa na nafasi mbalimbali.
ODM inataka ngome zake za jadi za kisiasa zilindwe katika mpango wa ushirikiano wa uchaguzi.
Suala la kutengewa maeneo limekuwa chanzo cha mvutano kati ya ODM na UDA.
ODM imekuwa ikitaka ngome zake ziheshimiwe, huku UDA ikitaka kila chama kiruhusiwe kuwasilisha wagombea katika maeneo yote isipokuwa kiti cha urais.
Gavana wa Mombasa na naibu kiongozi wa ODM Abdullswamad Nassir alisema suala hilo litashughulikiwa na kamati maalum ya vyama hivyo.
Suala la nani atakuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto 2027 pia limekuwa nyeti. Baadhi ya viongozi wa ODM tayari wamemuunga mkono Waziri wa Ushirika Wycliffe Oparanya kwa wadhifa huo.
Hilo limezua ushindani na washirika wa Naibu Rais Kithure Kindiki.
ODM inataka ushirikiano huo utoe nafasi ya chama kushiriki katika maamuzi muhimu kuhusu uchaguzi wa 2027.
Chama hicho pia kinataka kuwe na mpango wa pamoja wa kuelekea uchaguzi wa 2027.
Kiongozi wa wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohammed alisema mkutano huo utatoa mwelekeo kuhusu uchaguzi ujao.
“Kutakuwa na maamuzi mazito yatakayotoa mwelekeo wa kisiasa. Viongozi watatoa mwongozo wa kuelekea 2027,” alisema. Mpango huo unatarajiwa kuangazia mikakati ya kampeni, ushirikiano wa vyama na ujumbe wa serikali kwa wapigakura. ODM pia inataka kushiriki katika mjadala kuhusu Ruwaza mpya ya Rais Ruto ya 2060.
Rais anatarajiwa kuzindua mpango huo Agosti 12, siku moja baada ya kumalizika kwa mkutano wa Naivasha.
Mkutano huo pia unafanyika wakati ODM na UDA zinakabiliwa na ushindani wa kisiasa katika maeneo mbalimbali.
Mabadiliko ya uaminifu wa kisiasa, hasa Mlima Kenya, yameongeza presha kwa Rais Ruto.
UDA imepoteza baadhi ya washirika wake wakuu, wakiwemo magavana Irungu Kang’ata wa Murang’a na Kiarie Badilisha wa Nyandarua pamoja na Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro.
 Wakati huo huo, vuguvugu la Linda Mwananchi linalohusishwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna linaendelea kupanua mbawa zake.
 ODM ina wasiwasi kuwa vuguvugu hilo linaweza kupunguza nguvu zake katika baadhi ya ngome zake za jadi kuelekea uchaguzi wa 2027.