Ol Kalou: Gachagua sasa apaa huku Uhuru, Kindiki wakiyumba Mlimani
USHINDI mkubwa wa mgombea wa Democracy for Citizens Party (DCP), Sammy Kamau Ngotho, katika uchaguzi mdogo wa ubunge wa Ol Kalou umeibua mjadala mpya kuhusu mwelekeo wa siasa za Mlima Kenya kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Ngotho alipata zaidi ya asilimia 85 ya kura, huku mgombea wa UDA, Samuel Muchina Nyagah, akiambulia asilimia 13 pekee. Wagombea wengine saba waligawana asilimia mbili zilizosalia.
Kwa kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua, ushindi huo unampa nguvu mpya kisiasa na kumpatia mbunge wake wa kwanza katika Bunge la Kitaifa.
Hata hivyo, aliyekuwa Kamishna wa Mkoa Joseph Kaguthi amesema ushindi huo unaambatana na wajibu mkubwa.
“Ol Kalou ilikuwa kura ya maamuzi ya Mlima Kenya. Sasa Gachagua amepewa jukumu la kuongoza eneo hilo kuelekea 2027. Lazima awe kiongozi anayewaunganisha watu na asiwe wa kulipiza kisasi,” alisema.
Kaguthi alisema Gachagua anapaswa kusawazisha maslahi ya Mlima Kenya na yale ya taifa kwa ujumla.
Kwa Rais William Ruto, wachambuzi wanasema matokeo hayo yanatoa onyo kuhusu kupungua kwa ushawishi wake katika ngome iliyompa ushindi mkubwa mwaka 2022.
Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya alisema Rais anapaswa kujiuliza iwapo uamuzi wa kuunga mkono kuondolewa kwa Gachagua mamlakani mwaka 2024 ulikuwa sahihi.
“Ikiwa Rais atakuwa mkweli, lazima anajutia uamuzi huo kwa sababu ulisababisha mgogoro wa kisiasa unaozidi kukua kila siku,” alisema.
Mbunge wa Manyatta Gitonga Mukunji alisema ni jambo la kutia wasiwasi kwa UDA kupata asilimia 13 pekee katika eneo lililompa Rais Ruto takriban asilimia 87 ya kura mwaka 2022.
“Ukiangalia matokeo hayo, unaweza kudhani hata uungwaji mkono wa Rais katika uchaguzi wa urais unaweza kuwa chini zaidi,” alisema.
Kwa Naibu Rais Kithure Kindiki, wachambuzi wanasema matokeo hayo yanaonyesha bado hajakubalika kama mrithi wa Gachagua katika Mlima Kenya.
Mchambuzi wa siasa Gasper Odhiambo alisema Kindiki aliahidi kumshinda Gachagua Ol Kalou lakini akashindwa vibaya.
Alionya kuwa nafasi ya Kindiki kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto mwaka 2027 sasa inaweza kuwa hatarini.
Kindiki, hata hivyo, alisema ushindi wa Kenya Kwanza katika uchaguzi mdogo wa Mbeere Kaskazini na kushindwa Ol Kalou unamaanisha ushindani uko sare.
“Hii ni sare. Mechi ya mwisho ni mwaka 2027,” alisema.
Aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta pia amewekwa katika mizani kuhusu ushawishi wake Mlima Kenya baada ya chama chake cha Jubilee kupata kura 198 pekee.
Seneta mteule Karen Nyamu alisema Uhuru anapaswa kueleza kwa nini amekuwa akiunga mkono wagombea wa nje ya Mlima Kenya badala ya kukuza viongozi wa eneo hilo.