Pigo kwa Gachagua, korti yatupilia mbali kesi ya kutimuliwa serikalini, yamliwaza na Sh50m
ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua amepata pigo kubwa mahakamani, baada ya jopo la majaji watatu kutupilia mbali kesi ya kupinga kutimuliwa kwake serikalini.
Katika uamuzi wa majaji Freda Mugambi, Anthony Mrima na Eric Ogolla, walisema kwamba sheria zilifuatwa katika mchakato mzima wa kumtimua Bw Gachagua uongozini.
Jopo hilo, hata hivyo, lilisema mahali pekee Seneti ilipokosea ni kutompa nafasi ya kujitetea kibinafsi, haswa wakati alipougua na kukimbizwa katika hospitali ya Karen. Na kwa hilo, majaji wameafikia kumtunuku Sh50 milioni kama kiliwazo.
Mahakama ilikuwa imeorodhesha malilio sita ya Gachagua ambayo mawakili wake waliwasilisha wakitaka uamuzi bayana kuyahusu.
Nayo yalikuwa iwapo Mahakama Kuu ilikuwa na uwezo wa kisheria kusikiza kesi yake, kwamba kulikuwa na uonevu dhidi yake, iwapo umma ulihusishwa katika kutoa maoni, uhalali wa kanuni za bunge zilizotumiwa katika mchakato wa kumtimua, ufaafu wa Kithure Kindiki kuchukua wadhifa wake na iwapo Katiba ilifuatwa katika kumtimua.
Kuhusu kigezo cha uonevu na kutopewa nafasi ya kusikizwa, jopo la majaji watatu lilisema kukiukwa kwa haki hiyo hakuwezi kutumiwa kuharamisha kutimuliwa kwake.
Pia majaji hao walisema kuwa kumrejesha madarakani kutasababisha kuwe na manaibu rais wawili jambo ambalo haliwezani kisheria.
Ingawa hivyo, mawakili wa Bw Gachagua wakiongozwa na Paul Muite wamesema kuwa watakata rufaa kuhusu uamuzi huo.
Uamuzi huo sasa unaathiri kwa kiasi kikubwa nafasi yake ya kurejea katika ulingo wa kisiasa na kutimiza azma yake ya kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Bw Gachagua alikuwa akitarajia kubatilisha kuondolewa kwake madarakani hatua ambayo ingeimarisha hadhi yake ya kisiasa hasa Ukanda wa Mlima Kenya.
Badala yake, mahakama iliidhinisha uamuzi wa Bunge wa kumuondoa afisini na kupisha mrithi wake, Profesa Kithure Kindiki, kuendelea kuhudumu kama Naibu Rais.
Masuala mengine yaliyoamuliwa yalihusu iwapo kanuni za Bunge zilikuwa za kikatiba, iwapo taratibu za kikatiba zinazohusu kutimuliwa na za urithi wa uongozi zilifuatwa na iwapo Bw Gachagua alipatiwa haki ya kusikizwa.
Moja ya hoja kuu za Bw Gachagua ilikuwa kwamba wabunge na maseneta walikuwa tayari wameamua matokeo ya mchakato wa kumtimua kabla ya kumsikiliza.
Mahakama ilisema kuwa hakuna ushahidi wa moja kwa moja uliowasilishwa kuthibitisha madai hayo.
Kwa mujibu wa majaji, mwelekeo wa kisiasa pekee hauwezi kuchukuliwa kuwa upendeleo usio wa kikatiba.
“Katiba inakataza maamuzi yaliyokwisha kufanywa kabla ya kusikiliza suala husika,” jopo hilo lilisema.
Mahakama pia ilibaini kuwa Spika wa Bunge la Kitaifa na Spika wa Seneti walikuwa na jukumu la utekelezaji wa mchakato pekee na hawakuwa waamuzi wa mwisho kwa kuwa hawakupiga kura kuhusu hoja ya kumngátua Bw Gachagua.
Majaji kisha waligeukia suala la ushirikishaji wa umma, ambalo lilikuwa msingi na mojawapa wa maombi makubwa ya Bw Gachagua.
Walitupilia mbali madai kwamba umma ulikuwa umenyimwa fursa ya maana ya kushiriki katika mchakato huo.
Kambi ya Bw Gachagua ilidai kuwa mchakato huo uliharakishwa, huku wananchi wakipewa chini ya saa 48 na watu 200,000 pekee kushiriki.
Hata hivyo, mahakama haikukubaliana na hoja hiyo na ikabaini kuwa Bunge la Kitaifa lilitoa taarifa ya kutosha kupitia matangazo ya magazeti, njia mbalimbali za ushirikishaji wa umma na fursa halisi kwa wananchi kuwasilisha maoni yao.
Majaji walisisitiza kuwa Katiba inahitaji ushirikishaji wa maana wa umma na si lazima uwe wa asilimia mia moja.
“Ushirikishaji wa umma si hisani kutoka kwa Serikali bali ni haki ya kikatiba,” ikasema mahakama.
Jopo hilo pia liliamua kuwa Seneti haikulazimika kufanya zoezi tofauti la ushirikishaji wa umma kwa sababu jukumu lake katika mchakato wa kumbandua Bw Gachagua lilikuwa la kutoa uamuzi wa kisheria na si kutunga sheria.
Vilevile, mahakama ilikataa hoja kwamba ushirikishaji wa umma ulikuwa muhimu katika uteuzi na kuidhinishwa kwa Prof Kindiki kuwa Naibu Rais.