Serikali yalaumiwa kupuuza hali halisia ya kiuchumi kwa kurejesha e-Citizen kwa ulipaji karo
KUMEZUKA malalamiko mapya kufuatia uamuzi wa Rais William Ruto wa kufufua mpango wa malipo ya karo za shule kupitia mfumo wa e-Citizen, wakosoaji wakilaumu serikali kwa kupuuza hali halisi inayowakumba wazazi na shule nchini.
Wanaopinga mpango huo wamesema msimamo wa Rais wa kusisitiza utekelezaji wake unajiri licha ya upinzani kutoka kwa walimu wakuu, wazazi na mashirika ya elimu, pamoja na kesi inayoendelea katika Mahakama ya Rufaa kufuatia uamuzi wa Mahakama Kuu uliozima utekelezaji wa sera hiyo mwaka jana.
Akitetea agizo hilo Alhamisi, Rais Ruto alisema malipo ya kidijitali yataongeza uwazi na kupunguza mianya ya kupotea kwa fedha kwa njia ya pesa taslimu.
“Leo, mzazi anapaswa kulipa karo akiwa nyumbani kupitia e-Citizen, ambapo tunaweza kuthibitisha taarifa hizo. Nimeamua kimkakati kwamba, hatutaki tena kushughulika na fedha taslimu katika utawala huu kwa sababu pesa taslimu ni ngumu kufuatilia,” alisema katika mkutano wa pili wa elimu uliofanyika Naivasha.
Hata hivyo, wataalamu wa elimu na walimu wakuu wamesema hali halisi shuleni inafanya mpango huo kuwa mgumu kutekelezeka, kwa kuwa karo hulipwa kwa nyakati tofauti ilhali shule zinahitaji fedha za matumizi ya kila siku.
Mshauri wa sera katika shirika la Elimu Bora Working Group, Boaz Waruku, alisema shinikizo za serikali zinaonyesha kutojali changamoto za wananchi.
Alisema wazazi wa maeneo ya mashambani mara nyingi hulipa karo kwa njia mbadala kama kuni, chakula au kazi za mikono ili watoto wao waendelee kusoma licha ya ugumu wa kifedha.
“Mfumo wa e-Citizen unaweza kuwabana wazazi wanaolipa kwa njia ya mazao, kazi au makubaliano mengine na shule. Hali hii inaweza kuwafanya watoto kukosa elimu,” alisema.