Wanachama wa Sacco ya Safaricom wakodolea hasara ya Sh2bn ploti zilizonunuliwa kugeuka hewa
USIMAMIZI mbaya katika Kampuni ya Uwekezaji ya Safaricom (SIC) umewaweka wanachama wasiopungua 5,000 kwenye hatari ya kupata hasara ya Sh2 bilioni.
Haya yamejiri kufuatia miaka mingi ya usimamizi mbaya wa mamilioni ya pesa zilizokusanywa kutoka kwa wanachama na wateja, huku wanachama wa bodi wakiidhinisha ununuzi wa vipande hewa vya ardhi na viwanja visivyo na faida yoyote.
Shughuli za kimsingi za SIC zinahusu ununuzi wa vipande vya ardhi kisha kuviuza kuzalisha faida kwa wanachama wake na ujenzi wa nyumba za kuuza.
Chama hicho cha ushirika sasa kimeachwa kikiwa kimeshikilia ardhi inayokadiriwa kuwa na thamani ya Sh1.6 bilioni ambayo haijulikani ilipo kwa kuwa inapatikana vitabuni pekee, huku baadhi ya vipande vyake vikikwama kwenye miamba na vingine vinavyoandamwa na historia ya mafarakano ya kifamilia, vyote vikikosa wanunuzi.
Ukaguzi maalum ulioagizwa na wanachama wake 5,000 mwaka uliopita, ulimulika wanachama wa bodi hususan kwa kuidhinisha ununuzi wa mali isiyo na thamani yoyote na kukaidi ushauri wa kiufundi kuhusu kuongeza bei wakati wa kununua ardhi.
Ukaguzi huo ulibaini kwamba, huku ardhi ya SIC kufikia mwishoni mwa 2024 ikiripotiwa kuwa Sh2.64 bilioni, thuluthi mbili za mali hiyo zina utata au haziwezi kuuzika.
“Ukaguzi wa kina ulifichua kuwa ardhi yenye thamani ya Sh1,391,834,840 (asilimia 53 ya thamani ya mali yote kwa jumla) inazingirwa na utata kuhusu masuala anuai. Aidha, ardhi yenye thamani ya Sh245 milioni ilijumuisha vipande vya ardhi ambavyo vipo lakini, vinakabiliwa na changamoto zinazovifanya visiuzike,” ilisema ripoti.
Karibu nusu ya ardhi yenye utata ilikuwa hewa baada ya kuibuka baadhi ya maafisa walipitisha gharama za mwaka uliotangulia kama ardhi mpya, na kuongeza takriban Sh627 milioni kwa thamani ya ardhi inayomilikiwa na SIC bila ununuzi wowote mpya.
Wakaguzi mwaka uliopita walimshutumu mkaguzi aliyeajiriwa kutoka nje 2024 kwa kuongeza fedha hizo katika mali ya shirika hilo kuzua taswira kwamba mali ya ardhi iko juu, ilhali walihamisha gharama zilizosawiriwa kuwa za mwaka uliotangulia, lakini haikuwezekana kuzihusisha na mradi husika.
Suala hili limeibua maswali kuhusu uhalali wa faida za shirika hilo zilizotangazwa miaka ya mbeleni, kwa kuwa usimamizi wake umeanikwa kwa kuficha gharama ambayo, ikiripotiwa, itafuta faida.
Kwa mara ya kwanza katika miaka mitano, kampuni hiyo inatarajiwa kuripoti hasara kwa shughuli za kibiashara za 2025, na Mkutano Mkuu wa kila Mwaka (AGM) uliopangwa kufanyika mwezi uliopita ukilazimika kuahirishwa.
Ni wazi sasa kuwa faida ya zaidi ya Sh600 milioni zilizoripotiwa Kati ya 2021 na 2024 ni matokeo ya kuvuruga vitabu vya hesabu kuficha gharama na kuwahadaa wanachama kwamba yote ni shwari.