KPC yasema ilikubali mafuta mabovu kwa ruhusa ya Waziri Kinyanjui: ‘Alisema yachanganywe na mengine’
MENEJA Msimamizi wa Kampuni ya Mafuta Kenya Pipeline Pius Mwenda jana alisema kuwa kuna matukio mawili pekee ambapo mafuta yenye ubora wa chini yaliruhusiwa nchini.
Alisema ni mnamo 2019 ambapo tani 108,203 za mafuta yaliyokuwa yamesafirishwa kwa meli ya MT Ocean Tiara yalikataliwa kwa kukosa kutimiza vigezo.
Mnamo Machi 27, 2026, kampuni hiyo ilipata tani 60,000 za mafuta kwenye meli ya MT Paloma.
Mafuta hayo yalipimwa na yakakataliwa kwa sababu yalikuwa na kiwango cha juu cha madini ya Sulphur.
Hata hivyo, baadaye yaliruhusiwa na kuingizwa nchini kutokana na msamaha wa Waziri wa Uchukuzi, Lee Kinyanjui.
“Tulipata shehena hiyo mnamo Machi 27, 2026 na baada ya kuyapima mafuta hayo tuligundua yalikuwa na kiwango cha juu cha Sulphur. Hata hivyo, tulifuata amri ya Waziri Kinyanjui na kuruhusu mafuta hayo kulingana na maagizo yake.”
Maagizo hayo yako kwenye barua ya Machi 28, 2026 iliyoandikwa na Bw Kinyanjui alipokuwa amemweleza mwenzake Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi kuwa tani 60,000 za mafuta hayo hatari yalifaa yachanganywe na mengine yaliyokuwa yamehifadhiwa.
Kuchanganywa huko kungesaidia kupunguza kiwango cha juu cha Sulphur na Manganese katika mafuta yaliyokuwa katika MT Paloma.
Barua hiyo pia iliamrisha KPC na Mamlaka ya Kudhibiti Kawi (EPRA) idhibiti usambazaji wa mafuta hayo ikisubiri kuwasili kwa shehena nyingine Aprili 4.
“Kuwa KPC ikishirikiana na EPRA zidhibiti kusambazwa kwa mafuta hayo hadi shehena nyingine ya PMS iwasili mnamo Aprili 3 au 4 ambayo itatumika kupunguza kiwango cha juu cha madini ya manganese,” ikasema barua iliyowasilishwa jana mbele ya Kamati ya Kawi.
“Tulipokea barua kutoka kwa Waziri wa Biashara kuruhusu shehena hiyo kwenye mfumo wetu. Baadaye mafuta hayo yalitolewa kwa wanunuzi au kampuni za kuyauza mafuta.
“Mmiliki wa mafuta hayo hata hivyo aliambiwa aondoe bidhaa hiyo kutoka mtambo wa KPC. Hata hivyo ni bora ieleweke kuwa si jukumu la KPC kuyaharibu mafuta ya ubora wa chini ila ni la serikali ikishirikiana na sekta nyinginezo za kawi.”