Afya na Jamii

Kasoro ya kuzaliwa inayokumba watoto ambayo huja kugunduliwa baadaye

May 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KWA miaka mingi, wengi huifahamu nasuri kama tatizo linalowapata wanawake baada ya kushuhudia uchungu wa uzazi kwa muda mrefu pasipo usaidizi wa mhudumu wa afya aliyehitimu.

Lakini kuna aina adimu ya nasuri ambayo watu wachache huifahamu- ‘congenital ureteric fistula’ ambayo mtoto huzaliwa nayo.

Kwa Virginiah Wanjira, safari ya kuelewa hali ya binti yake mwenye umri wa miaka mitano haijakuwa rahisi.

Binti yake alizaliwa kawaida bila changamoto zozote zilizoonekana.

Lakini alipofikisha umri wa kwenda shule, Virginiah alianza kuona jambo lisilo la kawaida.

“Nilikuwa na wasiwasi kwa sababu kila aliporudi kutoka shule alikuwa amelowa. Nilijua kuna umri mtoto hafai kuwa akijikojolea ila yake ilikuwa tofauti. Nikaanza kutafuta msaada kwa sababu niliona si jambo la kawaida,” anasema.

Anaeleza kuwa alijaribu mbinu kadhaa na hata kutafuta matibabu katika zahanati mbalimbali bila kupata usaidizi.

“Nilitumwa katika hospitali ya Kenyatta Narobi ila kwa sababu natoka Murang’a, sikuwa na nauli.”

Baada ya vipimo vya kina ikiwemo ambavyo vilijumuisha uchunguzi wa figo, mrija wa mkojo na ureta, ilibainika mtoto huyo alikuwa na tatizo adimu la aina ya nasuri inayofahamika kama congenital ureteric fistula, ambapo alizaliwa na mirija minne ya mkojo badala ya miwili ya kawaida; moja katika upande wa kulia na nyingine upande wa kushoto wa figo.

Hali hiyo ilisababisha mkojo kuvuja.

Kwa mujibu wa muuguzi Solomon Olale, anayeshughulikia wagonjwa wa nasuri kutoka Flying Doctors Society of Africa, hali hiyo ni nadra sana.

“Katika miaka yangu minne ya kazi nimekumbana na visa vinne pekee vya hali hii. Ni tatizo la kuzaliwa nalo na wengi hawalifahamu. Kwa mtoto huyu, mirija hiyo itaunganishwa kwa upasuaji ili kurekebisha hitilafu,” anasema.

Dkt Olale anasisitiza umuhimu wa kliniki wakati wa ujauzito.

“Ili kuepuka masuala kama hayo, wazazi wasikose kwenda kliniki na wakiwa pale, wanafaa kuwa wazi na kuelezea chochote kinachosumbua mtoto. Kando na hayo, vipimo vya ujauzito vinaweza kusaidia kubaini changamoto nyingi za kuzaliwa,” anasema.

Kwa Virginiah, safari ya kutafuta tiba haikuwa rahisi.

Alizunguka hospitali kadhaa, zikiwemo Othaya na Kenyatta, lakini changamoto za kifedha zilimuandama.

“Nilikuwa nimekata tamaa kabisa. Niliambiwa niende Kenyatta lakini sikuwa na uwezo. Nilihisi nimefika mwisho,” anasema.

Matumaini yake yalirejea aliposikia kupitia vyombo vya habari kuhusu uchunguzi unaofanywa bila malipo wa nasuri katika Hospitali ya Rufaa ya Murang’a.

“Nilienda pale nikiwa sina matumaini, lakini nikapata msaada,” Virginiah anasema kwa furaha.

Simulizi ya Virginiah inafichua sura nyingine ya nasuri ambayo mara nyingi hufichwa kwa sababu ya aibu, ukosefu wa maarifa na kutafuta matibabu kuchelewa.

Katika mpango huo wa kusaidia walioathirika na nasuri Murang’a mnamo Aprili 18, 2026, wanawake na wasichana 449 walifanyiwa uchunguzi, ushauri, tiba ya viungo na upasuaji wa kurekebisha nasuri mbali mbali.

Mpango huo ulileta pamoja serikali ya Kaunti ya Murang’a, Wizara ya Afya, M-Pesa Foundation, Flying Doctors na Amref Health Africa.

Muuguzi na mkufunzi wa aina ya nasuri inayofahamika kama Vesicovaginal Fistula (VVF), Christine Muthengi, anasema baadhi ya wagonjwa wameishi na hali hiyo kwa miongo kadhaa.

“Kuna waliopata nasuri tangu miaka ya 1990. Wameachwa na waume, kutengwa na jamii na wengine wamejificha kwa sababu ya aibu,” anasema.

Anaeleza kuwa nasuri ya uzazi bado ni changamoto kubwa, hasa kwa wanawake katika maeneo yasiyo na huduma bora za uzazi.

“Nasuri haisababishi tu mtu kuvuja mkojo. Ni majeraha ya mwili, akili na utu. Wanawake wengi huishi kwa fedheha kubwa,” anasema.

Kwa mujibu wa wataalamu, Kenya ina takriban wanawake 120,000 ambao bado hawajapata matibabu ya nasuri.

Ingawa nasuri nyingi huhusishwa na uchungu wa muda mrefu wa uzazi bila huduma ya dharura, pia kuna aina nyingine mbalimbali za ugonjwa huu.

Aina za nasuri

Kuna aina ya nasuri ambapo nafasi ya wazi hujitokeza baina ya uke na kibofu cha mkojo. Kulingana na madaktari aina hii ya nasuri imekithiri sana.

Aina nyingine ni nafasi ya wazi isiyo ya kawaida baina ya uke na mifereji inayobeba mkojo kutoka kwa figo hadi kwenye kibofu.

Pia kuna nasuri ambapo pengo hujitokeza baina ya uke na mrija unaobeba mkojo kutoka mwilini.

Aina nyingine ni nafasi ya wazi kati ya uke na sehemu ya chini ya rektamu.

Pia kuna nasuri inayosababishwa na pengo kati ya uke na utumbo mpana.

Kuna aina nyingine ya nasuri ambapo kuna pengo baina ya uke na mfumo wa mmeng’enyo wa chakula.

Bi Muthengi anasema changamoto kubwa si ukosefu wa matibabu pekee, bali unyanyapaa.

“Wanawake wengi huficha hali yao kwa hofu ya kudharauliwa na kuchekwa. Wengine hawajui hata ni ugonjwa unaotibika,” anasema.

Hata katika kaunti kama Murang’a yenye viwango vya juu vya kina mama kujifungua hospitalini, umasikini, ujauzito wa mapema na kuchelewa kupata huduma za dharura bado huchangia tatizo hilo.

Kwa mujibu wa Patricia Ithau, msimamizi wa M-PESA Foundation, matibabu ya nasuri yanabadilisha maisha.

“Huenda upasuaji ukaonekana mdogo, lakini huimarisha utu, afya na mustakabali wa mwanamke kwa namna kubwa sana. Hakuna mwanamke anayepaswa kuumia kimya kimya,” anasema.

Kupitia uwekezaji wa Sh8.1 milioni katika mpango huu ukiwa sehemu ya mpango mpana wa Sh213 milioni, zaidi ya wanawake 1,500 katika kaunti zilizoathirika wamepata matibabu.

Muuguzi Olale anawahimiza wazazi kuwa makini pale watoto wanapoonyesha dalili zisizo za kawaida kama kujikojolea kila mara.

“Mzazi akiona mtoto anaendelea kujikojolea bila sababu maalum, asipuuze. Tafuta ushauri wa kitabibu mapema. Utambuzi wa mapema huokoa maisha na mateso,” anasema.