Afya na Jamii

Kinachofanya watoto wengi kudumaa wakikua licha ya juhudi za miaka 30

Na LINET OWOKO April 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

NI asilimia tatu tu ya watoto wenye umri wa miezi 6–23 katika maeneo yenye uhaba mkubwa wa chakula nchini Kenya wanaopata lishe ya kutosha, Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema, likifichua pengo kubwa la lishe ya watoto licha ya maendeleo ya kitaifa katika kupunguza kudumaa kwa kipindi cha miaka 30 iliyopita.

WHO inafafanua kudumaa kama hali ya mtoto kuwa mfupi kuliko umri wake, na ni kiashiria muhimu cha utapiamlo wa muda mrefu.

Kwa jumla nchini, asilimia 31 ya watoto katika kundi hilo hupata lishe chini ya kiwango kinachokubalika, huku asilimia 37 pekee wakipata mlo wenye aina mbalimbali za vyakula.

Ingawa asilimia 90 ya watoto nchini Kenya hunyonyeshwa, ni asilimia 61 pekee wanaonyonyeshwa maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya kwanza kama inavyopendekezwa.

Takwimu hizi zinaakisi kiwango cha kudumaa nchini ambacho ni asilimia 18, kikipungua kutoka asilimia 40 mwaka 1993.

Hata hivyo, maendeleo haya ya kitaifa yanaficha tofauti kubwa kati ya kaunti.

Kaunti ya Kilifi ina kiwango cha kudumaa cha asilimia 37, ikifuatiwa na Pokot Magharibu (asilimia 34) na Samburu (asilimia 31), viwango vinavyofanana na wastani wa kitaifa wa miaka 30 iliyopita.

Kwa upande mwingine, Kisumu na Garissa zina viwango vya chini vya takriban asilimia 9.

Tofauti kati ya kaunti zilizo juu na zilizo chini sasa ni kubwa kuliko pengo kati ya wastani wa Kenya na baadhi ya nchi tajiri.

Mkurugenzi mtendaji wa SUN CSA Edgar Okoth, alionya dhidi ya kuridhika na kupungua kwa wastani wa kitaifa.

Alisema ingawa kupungua kwa kudumaa ni jambo la kupongezwa, tatizo hilo haliwezi kurekebishwa baada ya kutokea.

Alisisitiza kuwa lengo linapaswa kuwa kuondoa kabisa kudumaa, si kupunguza tu takwimu.

Pia, tofauti za kiuchumi zinaonekana wazi. Kudumaa huathiri asilimia 28 ya watoto katika kundi la chini la kipato, ikilinganishwa na asilimia 9 ya watoto katika kundi la juu.

Aidha, asilimia 22 ya watoto wenye mama wasio na elimu rasmi wamedumaa, dhidi ya asilimia 9 ya wale wa mama waliofikia elimu ya sekondari au zaidi.

Takwimu nyingine zinaonyesha kuwa asilimia 10 ya watoto chini ya miaka mitano ni wenye uzito mdogo, asilimia 5 wamedhoofika kiafya kutokana na utapiamlo mkali, na asilimia 3 wana uzito uliozidi.

Kujibu changamoto hizi, Wizara ya Afya kwa usaidizi wa WHO ilitengeneza mwongozo wa kitaifa wa kuzuia na kudhibiti utapiamlo mkali mwaka 2025 pamoja na nyenzo za mafunzo kwa wahudumu wa afya.

Mwaka huo pia wakufunzi 25 wa kitaifa walithibitishwa, na baadaye wahudumu 30 kutoka Siaya na Homa Bay walipewa mafunzo.