Wataalam wasema bangi huchangia mtu kusimulia vitu akilini ambavyo havikutokea
UTAFITI mpya umebaini kuwa matumizi ya bangi yanaweza kuathiri kumbukumbu kwa kusababisha mtu kufikiria matukio ambayo hayakuwahi kutokea.
Utafiti huo uliofanywa na watafiti kutoka Washington State University na kuchapishwa katika jarida la Journal of Psychopharmacology, unaonyesha kuwa kando na kumfanya mtu kusahau, kutumia bangi pia hubadilisha ukweli katika kumbukumbu ya mtu.
Katika utafiti huo uliowahusisha watumiaji 120 wa bangi, washiriki walipewa bangi yenye kemikali ya THC au dawa bandia isiyo na kemikali hiyo.
Baadaye walifanyiwa majaribio ya kumbukumbu ya maneno, picha na matukio.
Matokeo yalionyesha kuwa karibu asilimia 70 walipata matatizo ya kumbukumbu baada ya kutumia THC.
Hata hivyo, jambo lililowashangaza watafiti ni kuwa baadhi ya washiriki walikumbuka kwa uhakika mambo ambayo hayakuwa ya kweli.
Hali hii inajulikana kama “kumbukumbu za uongo,” ambapo ubongo hujaribu kujaza mapengo ya kumbukumbu kwa taarifa zisizo sahihi lakini zinazoonekana kuwa halisi.
Watafiti wanaeleza kuwa THC huathiri sehemu za ubongo zinazohusika na kuhifadhi na kurejesha kumbukumbu, hivyo kufanya kumbukumbu kuwa dhaifu na zisizo sahihi.
Aidha, bangi ilionekana kuathiri aina mbalimbali za kumbukumbu, ikiwemo ya maneno, picha na matukio, pamoja na uwezo wa kukumbuka mipango ya baadaye.
Kwa kuzingatia kuwa bangi ndiyo dawa ya kulevya inayotumika zaidi nchini Kenya, wataalamu wanaonya kuhusu athari zake kwa afya ya akili.
Utafiti huu unaonyesha haja ya tahadhari zaidi, hasa miongoni mwa vijana, kwani hata matumizi ya kiwango kidogo yanaweza kuathiri kumbukumbu na uamuzi wa mtu.