Akili Mali

Faida za mtambo wa kukoboa nafaka kwa wakulima wa pato dogo vijijini

Na RICHARD MAOSI June 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SEKTA ya kukuza aina mbalimbali ya nafaka za thamani ya juu kama vile mpunga, mahindi, maharagwe, pojo, si rahisi hususan miongoni mwa wakulima wenye kipato kidogo vijijini.

Shadrack Ikunga kutoka kijiji cha Kilimu, Kaunti ya Kitui anasema licha ya changamoto hizi nyingi, biashara ya nafaka humlipa mkulima hela nzuri.

Hata hivyo, mkulima anastahili kuzingatia utaratibu wa kupanda, kupalilia na kuvuna bila kusahau matumizi ya mbegu safi zilizoidhinishwa na wanasayansi.

Anasema kwa kutumia mtambo wa ‘Thresher’ biashara yenyewe itapata manufaa zaidi ikiwa ni hatua inayoonyesha kuyaelewa maelekezo ya kiufundi kufanikisha kilimo biashara.

Aidha anasema wakulima wengi huyakoboa mazao yao kwa kutumia mikono jambo linalofanya baadhi ya mazao kupotea kwa sababu ya kuharibika.

“Baadhi ya wakulima wanategemea viwanda ili kuyakoboa mazao yao na matokeo yake huishia kupata hela ndogo sana ambazo hazilingani na gharama ya uzalishaji,” anasema.

Mataifa ya Afrika mashariki kwa mfano hutegemea nafaka mbalimbali kwani ndizo huendesha uchumi wao.

Akiwa mtaalam wa aina mbalimbali ya mitambo ya kilimo, amekuwa akiweka mkazo kwa wakulima kujitahidi ili kuyakoboa mazao yao kwa kutumia mitambo kabla ya kufika sokoni.

“Kwanza humpatia mkulima hela nzuri na pia huwa na soko hakika hasa miongoni mwa mikahawa mingi mijini ambayo huhitaji bidhaa hizi kwa wingi. Pili huzingatia kiwango cha juu cha usafi wa chakula.”

Kulingana na Ikunga, mtambo wa ‘Thresher’ una faida tele ikiwa ni pamoja na uwezo wa kukoboa na kusaga nafaka kwa wakati mmoja.

“Mtambo huo hurahisisha kazi ya mikono na kupunguza gharama za umeme. Husaga vitu vingi kama mahindi, mchele, ulezi, mihogo, kahawa na nafaka zote zikiwa kavu ambapo katika hatua ya kwanza huwa ni kukokoboa nafaka.”

Mtambo huo una uwezo wa kusaga zaidi ya kilo 300 kwa saa na hutumia umeme mdogo wa majumbani.

Anasema ingawa wakulima wengi msimu huu wanalia wa sababu ya bei ya chini ya kilo 90 ya mahindi, tumaini lao kubwa ni kwamba wanaweza kuhifadhi mazao yao wakisubiri bei kuimarika sokoni.

Kwa kutumia aina hii ya zana wanaweza kuyakoboa na hatimaye kuyahifadhi mazao yao katika maghala wakisubiri bei ipate kuimarika sokoni.

Anasema mtambo huu wa ‘thresher’ huwafanya wakulima wasikue na haraka ya kuuza nafaka zao kwa bei ya chini kwa kuhofia kuharibikiwa na mazao.

Kinyume na miaka ya awali ambapo wakulima wengi walikuwa wakitumia miti kutwanga mahindi yao mara tu baada ya kuvuna mitambo ya aina hiyo sasa inasaidia.

Mbinu yeyewe haikuwa faafu kwa sababu wakati mwingi ilichangia kuharibika kwa ubora wa mahindi.

Anasema mtambo huu umebainika kuwa wa manufaa makubwa kwa wakulima wadogo kutoka kaunti ya Kitui.

Kaunti hiyo hukuza zaidi pojo miongoni mwa nafaka nyinginezo kwa wingi.

Kwa sababu hiyo biashara ya kukoboa na kusaga nafaka aina ya dengu hususan miongoni mwa vijana inazidi kupata umaarufu.

Baadhi yao wameungana na kutengeneza makundi ya ushirika, wakachukua mikopo na kujinunulia ‘thresher’ ndogo kwa ajili ya kuwafaa wakulima.

Kwa kumiliki mtambohuo, wapo wafanyabiashara wanaojihusisha na kununua nafaka kama mahindi na mpunga halafu huenda kukoboa au kusaga.

Biashara ya kukoboa na kusaga mahindi kwa mfano ni maarufu sana jijini Nairobi hasa maeneo ya Viwandani almaarufu Industrial Area.

“Mbinu na mikakati mipya ya kutumia mitambo ya kiteknolojia pia humwezesha mjasiriamali kuzifungasha katika ubora wa hali ya juu. Kuwa na nemboyako mwenyewe iayokutambulisha kibiashara,” anaongeza.