Wakili wa Besigye anyakwa kabla ya kumkabidhi Muhoozi hati ya mahakama
KAMPALA, Uganda:
MAAFISA wa usalama Uganda Jumanne, Juni 16, 2026 walimkamata mwanasiasa wa upinzani Erias Lukwago ambaye pia ni wakili wa Kiongozi wa PFF na mwanasiasa mkongwe Kizza Besigye.
Besigye anaendelea kuzuiliwa baada ya kushtakiwa kwa kosa la uhaini nchini humo huku afya yake nayo ikiendelea kudorora korokoroni.
Lukwago, ambaye zamani alikuwa meya wa Kampala, pia anamwakilisha Besigye katika kesi nyingine dhidi ya Mkuu wa jeshi la Uganda, Muhoozi Kainerugaba.
Katika kesi hiyo, Besigye amemshtaki Kainerugaba, mwanawe Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, kwa kutishia maisha yake mara kwa mara kupitia mitandao ya kijamii.
Katika ujumbe uliowekwa kwenye mtandao wa X, PFF ilisema kuwa Lukwago alitiwa mbaroni nyumbani kwake.
“Tunapenda kuufahamisha umma kwamba mwenyekiti wetu wakili Erias Lukwago, ametekwa nyara na maafisa wa polisi na kupelekwa mahali kusikojulikana. Tunahofia sana usalama wake kwa sababu hatujui yuko wapi,” ukasema ujumbe wa chama hicho mitandaoni.
Kiongozi wa upinzani mwanasiasa msanii Bobi Wine, ambaye kwa sasa yuko uhamishoni Amerika, alisema kupitia X kwamba wanajeshi waliokuwa wakitekeleza maagizo ya Kainerugaba ndio walimkamata Lukwago.
Kukamatwa huko kulitokea wakati Lukwago alikuwa akijiandaa kumkabidhi Kainerugaba nakala ya hati ya korti kwenye kesi anayomwakilisha Besigye.
Reuters haikuthibitisha madai haya kwa njia huru kwa kuwa msemaji wa jeshi hakujibu jumbe na simu alizopigiwa.
Kainerugaba, anayejulikana sana Uganda kwa machapisho yake yenye utata kwenye mitandao ya kijamii, amekuwa akitishia mara kwa mara viongozi wa upinzani na hata kutumia lugha ya uchochezi na chafu dhidi yao.
Wine, kiongozi wa chama cha NUP, chama kikuu cha upinzani Uganda, alitorokea uhamishoni baada ya kupoteza uchaguzi mkuu wa mnamo Januari. Hii ni baada ya Kainerugaba kutishia kuwa angemuua kutokana na mzozo uliotokota baada ya ushindi wa Rais Museveni mnamo Januari mwaka huu.
Jumatatu, Kainerugaba aliandika kwenye X kwamba angemkamata mtu yeyote ambaye angejaribu kumkabidhi nakala za hati za mahakama.
Kutokana na mtindo wake na kiburi kingi, wengi wamekuwa wakifasiria kuwa Kainerugaba yupo juu ya sheria.
Aliongeza kuwa alikuwa “amemkamata mpumbavu mmoja na kumpeleka kwenye sehemu ya chini ya jumba lake.”
Baadaye, alichapisha picha ya mtu aliyefanana na Lukwago akionekana mwenye hofu kubwa, akiwa ameweka viganja vya vidole usoni mwake.
Katika chapisho jingine, alisema alikuwa anajivunia maumivu na mateso yote ambayo angewasababishia viongozi wa upinzani aliowarejelea kama wahalifu kama Lukwago.
Mnamo Mei 2025, Kainerugaba alidai kuwa alikuwa akimzuilia kiongozi mmoja wa upinzani aliyekuwa ametoweka na akatishia kumhasi.