Habari Mseto

Supkem yaalani kuvamiwa kwa mkutano wa bajeti kanisani

Na CECIL ODONGO June 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BARAZA Kuu la Waislamu Nchini (SUPKEM) jana lililaani tukio la kuvamiwa na kuvurugwa kwa mkutano wa kupiga msasa bajeti, uliofanyika katika kanisa la All Saints Cathedral jijini Nairobi.

Supkem ilirejelea tukio hilo kama kitendo kisichokubalika cha kutovumiliana kisiasa, likitaka hatua za haraka zichukuliwe dhidi ya wwatu wote waliohusika.

Mkutano huo ulikuwa wa kujadili athari za bajeti ya kitaifa ya 2026-27 kwa mwananchi wa kawaida baada ya kusomwa na Waziri wa Fedha John Mbadi wiki jana.

Kikao hicho kilihudhuriwa na makundi mbalimbali yakiwemo viongozi wa mashirika ya kiraia, viongozi wa kidini, mawakili na raia.

Ripoti ziliarifu kuwa kundi la watu lilivamia mkutano na kuzua vurugu hali iliyolazimu polisi kuingilia kati.

Kwa mujibu wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS), maafisa waliitikia haraka baada ya kupokea taarifa.

NPS ilisema polisi wameanza uchunguzi na wanapitia kanda za kamera za CCTV ili kubaini na kuwakamata watu wengine wanaohusishwa na ghasia hizo.

Huduma hiyo pia imeomba wananchi kutoa taarifa zozote zitakazosaidia uchunguzi kupitia vituo vya polisi na njia zingine rasmi.

Katika taarifa yake Supkem ilieleza kusikitishwa na kisa hicho.

“Kinachosikitisha zaidi ni ujasiri walioonyesha kuvamia wakiwa na nia ya kuumiza washiriki,” Supkem ilisema ikiongeza kuwa uvamizi wa eneo la ibada ni ukosefu wa heshima kwa asasi za kidini.

“Supkem inaitaka hatua za haraka na madhubuti zichukuliwe dhidi ya wahusika na watu waliowatuma,” ikaongeza.

Baraza hilo lilisisitiza kuwa teknolojia ya kisasa ya ufuatiliaji wa matukio inapaswa kusaidia wachunguzi kubaini waliohusika.

“Kupitia teknolojia ya kisasa, picha za CCTV za tukio hili zinatoa ushahidi wa kutosha kwa wachunguzi wa polisi kuwafuatilia waliohusika na kuwawajibisha.”

Supkem, pia ilionya kuhusu kuongezeka kwa vurugu na makabiliano katika mikutano ya kisiasa nchini.

“Ghasia hizo zikiendelea basi tutajipata katika hali inayofanana na ile ya kuelekea uchaguzi wa 2007,” ikasema taarifa hiyo.