• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 7:05 PM
KINAYA: ‘Ouru’ ni sungura mjanja, huenda ateme ‘baba’ baada ya kumtumia

KINAYA: ‘Ouru’ ni sungura mjanja, huenda ateme ‘baba’ baada ya kumtumia

Na DOUGLAS MUTUA

NIMEKWAMBIA kwa muda lakini umekataa kuniamini.

Utaniamini hili likitokea. Naamini hatimaye ‘Ithe wa Jaba’ atalipa deni la Daktari Kipchirchir Samoei.

Huamini kwa kuwa umemwona mwenyeji huyo wa Ikulu akitema cheche za matusi na kuwaonya wafuasi wake ‘wasimbebe kitoto’.

Mengine hayaandikiki, nitakoma hapo.

Mwana wa Jomo ni sungura mjanja. Anampumbaza ‘Baba’ ili aweze kutawala kipindi chake cha pili kwa amani.

Hata mimi ningefganya hivyo ningekuwa kinara mkuu wa Kenya. Unataka kuniambia ungetaka kupigiwa kelele kila saa na dakika, kukumbushwa eti hukuchaguliwa kihalali?

Kila mlala kasri anapenda amani yake.

Anapenda uhakika kwamba leo na kesho ndiye mwenyeji humo, asiamshwe usiku na nduru eti wasiompenda wamekuja kumtimua!

Anapenda kupendwa pia, si kutolewa vitisho vya watu milioni moja kuandamana kutoka Bustani ya Uhuru Park hadi Ikulu kummwamsha awakumbushe aliingiaje humo.

Tuambizane ukweli: Wakati unafika ambapo kila mtu anajali maslahi yake, ikiwa ni mbio unaambia mguu niponye, ujinusuru peke yako.

‘Ithe wa Jaba’, alijua fika kwamba ikiwa kuna wa kutolewa Ikulu na wale mabwana waliokuwa njiani kwenda Kanaani ya kufikirika ila safari yao ikavunjika, ni yeye.

Si Dkt Samoei. Huyo na mkewe na watoto wanalala Karen, karibu na ‘Baba’, na hujui usiku majirani hao wanaambiana nini.

Labda wanaombana moto wa kupikia chai.

Ukiingia Ikulu unakuwa mfungwa wa taifa kwa miaka mitano, ukibahatika zaidi unadumu humo miaka 10 kamili. Jela ya hiari eti.

Hii ina maana ‘Baba’ na wafuasi wake wangepandwa na wa kwao baada ya kushtuliwa na mamba wa ‘Mto Jordan’, waamue kuingia Ikulu kwa kifua, wangempata Jomo mdogo.

Hata wewe hungetaka kukutwa peke yako na wehu wakuhangaishe ilhali unadai kusimamia nchi kwa usaidizi wa mdogo wako.

Unatumia akili kujiokoa.

Si ajabu tuliambiwa ‘hendisheki’ au ‘handisheki’ ni makubaliano ya watu wawili – ‘Ithe wa Jaba’ na ‘Baba’ – na wala si ya nchi nzima.

Hata hivyo, kwa kuwa ‘Baba’ huota ndoto ya mzee wake ya kuongoza Kenya angalau kwa siku moja pekee, anadhani ‘hendisheki’ ni zaidi ya hapo.

Atajilaumu mwenyewe.

Ndiposa mambo anayosema kama ya kura ya maoni kuhusu Katiba ili nafasi zaidi za uongozi ziundwe yamenyamaziwa na kutizamwa kwa mbali na ‘Ithe wa Jaba’.

Wajua, hali ilivyo sasa ni rahisi sana kwa ‘Ithe wa Jaba’ kumcheza shere ‘Baba’ bila kuathirika vibaya kwa namna yoyote ile.

Anachohitaji ni kumwambia ‘mzee umekwenda mbio sana, punguza kasi lau sivyo ukanyange nje’, naye ‘Baba’ kwa hasira awatangazie Wakenya ‘hendisheki’ imevunjika!

Kisha? Aanzishe maandamano ya kumlaumu kiongozi wa nchi kwa kumsaliti, amtukane atakavyo, atangaze atakiona cha mtema kuni 2022!

Kumbuka hiyo 2022 Ouru hawanii.

Huku hayo yakiendelea, anachoweza kufanya ‘Ithe wa Jaba’ ni kutupa mikono hewani na kusema ‘hata sijui ni shetani yupi aliyeniingia akilini nikampuuza Dkt Samoei’.

Halafu? Amwambie Dkt Samoei ajongee, washikane mikono na kuendelea na safari ya 2022 walipoisitishia.

Binafsi naamini ‘Ithe wa Jaba’ anakasirika akiona yeyote kutoka mlimani akijipendekeza kwa Dkt Samoei kwani anataka yeye mwenyewwe amteulie mgombea mwenza huko.

[email protected]

You can share this post!

DINI: Ulimi unaolalamika ni dhihirisho la moyo usiotosheka,...

Simhitaji Raila 2022 – Kalonzo

adminleo