Makala

Maelfu hatarini Kenya ufadhili wa vita dhidi ya Ukimwi ukididimia

Na ANGELINE OCHIENG April 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI ya Kenya inakabiliwa na hali tata katika juhudi zake za kuzuia maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (HIV) kufuatia kupunguzwa kwa ufadhili kutoka Amerika, hatua inayotishia kufuta mafanikio yaliyopatikana kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita.

Mpango wa tohara ya hiari kwa wanaume (VMMC), ambao umekuwa nguzo muhimu ya kupunguza maambukizi ya HIV, umeathirika pakubwa baada ya kuondolewa kwa msaada kutoka Mpango wa Dharura wa Rais wa Ameria wa Kupambana na Ukimwi (PEPFAR) mnamo Septemba 2025.

Aidha, pendekezo la Amerika la kusitisha ufadhili wa kondomu na mpango wa uzazi nchini limeongeza presha katika sekta ya afya.

Kwa sasa, Kenya inahitaji kondomu milioni 400 kila mwaka, lakini serikali husambaza takriban 200 milioni pekee.

Nusu iliyosalia ilikuwa ikifadhiliwa na wafadhili, hasa USAID. Hata hivyo, pengo la takriban Sh803 milioni sasa halijazibwa, jambo linalohatarisha juhudi za kudhibiti maambukizi mapya.

Changamoto hizi zinajitokeza wakati ambapo takwimu zinaonyesha kupungua kwa kasi ya tohara ya wanaume tangu mwaka 2020.

Ingawa zaidi ya wanaume 2.6 milioni wamefanyiwa tohara tangu 2007, idadi ya wanaojitokeza kwa huduma hiyo imeendelea kushuka, hali inayoongeza hatari ya kuongezeka kwa maambukizi mapya ya HIV.

Kwa mujibu wa Meneja wa Mpango wa Vijana katika NASCOP, Bw Ambrose Juma, baadhi ya kaunti zimepunguza kipaumbele cha huduma hiyo, huku wataalamu wakihamishwa katika vituo visivyotoa huduma za tohara.

Aidha, vifaa muhimu vinakosa kutumika hadi vinaharibika.

“Tunaendelea kushuhudia kushuka kwa huduma hata katika maeneo yenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya HIV. Hii ni hatari kwa afya ya umma,” alisema Bw Juma.

Kwa upande wa kimataifa, kampuni kubwa ya kutengeneza kondomu duniani, Karex ya Malaysia, imetangaza kuongeza bei ya bidhaa zake kwa hadi asilimia 30 kutokana na changamoto za upatikanaji wa malighafi, hali inayoweza kuongeza gharama kwa watumiaji nchini Kenya.

Takwimu za hivi punde zinaonyesha kuwa watu 54 huambukizwa HIV kila siku nchini Kenya, huku 57 wakifariki kutokana na magonjwa yanayohusiana na Ukimwi.

Aidha, maambukizi mapya yaliongezeka kutoka 16,752 mwaka 2024 hadi 19,991 mwaka 2025.

Wataalamu wanaonya kuwa bila hatua za haraka, pengo la ufadhili na kupungua kwa huduma muhimu kama tohara na usambazaji wa kondomu vinaweza kusababisha ongezeko kubwa la maambukizi mapya, na hivyo kurudisha nyuma juhudi za taifa katika vita dhidi ya Ukimwi.

Maelezo ya ziada: Benson Matheka