Habari za Kitaifa

Ndege ya KDF yaanguka na kushika moto, watu watano wathibitishwa kufariki

April 18th, 2024 1 min read

Na CAROLINE WAFULA

NDEGE ya Jeshi la Kenya imeanguka na kushika moto katika eneo la Sindar, lokesheni ya Kaben kwenye mpaka wa kaunti za Elgeyo Marakwet na Pokot Magharibi, na kuua abiria watano papo hapo, Kamanda wa Kaunti Peter Mulinge amethibitisha.

Taifa Leo imethibitisha pia kwamba Mkuu wa Majeshi Francis Ogolla alikuwa miongoni mwa waliokuwa ndani ya helikopta hiyo iliyohusika katika ajali.

Watu watatu wameponea wakiwa na majeraha na wamekimbizwa hospitalini kupitia kwa ndege nyingine ya KDF.

Ndege hiyo iliyokumbwa na mkasa ilikuwa na watu wanane, na ilianguka mwendo wa saa nane na dakika hamsini.

Ndege hiyo ilikuwa miongoni mwa zingine tatu na ilikuwa inaondoka eneo la Cheptulel Pokot Magharibi, kulingana na Kamanda wa Kaunti. Ilikuwa ya kwanza kupaa, kabla ya kuanguka dakika chache baadaye.

Habari zaidi ni kadri tunavyozipokea….