Siasa

Jamii ya Mulembe nao wasema watadai kiti cha Unaibu Rais kuelekea kura 2027

Na ERIC MATARA May 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI kutoka Magharibi mwa Kenya sasa wanamtaka Rais William Ruto amchukue Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi au Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula kama mgombea-mwenza katika uchaguzi mkuu wa 2027.

Zaidi ya viongozi 30 waliochaguliwa, waliokutana Jumapili katika hoteli moja mjini Naivasha, pia walitangaza kuwa watamuunga mkono Rais Ruto ili achaguliwe tena.

Tangazo hilo linamweka Rais Ruto katika hali ngumu zaidi, huku nafasi ya Naibu Rais Kithure Kindiki ikiwa ndiyo inayowaniwa zaidi.

Maeneo ya Nyanza na Pwani pia yanachemelea nafasi ya Profesa Kindiki.

Katika taarifa ya pamoja iliyosomwa na Mbunge wa Lugari, Nabii Nabwera, viongozi hao walisema wakati umefika ambapo eneo hilo linastahili kupata nafasi hiyo ya hadhi serikalini.

“Sisi viongozi kutoka Magharibi tunamuunga Rais Ruto achaguliwe tena mnamo 2027. Eneo letu limeshuhudia maendeleo mengi na tutanufaika akiendelea kukaa mamlakani,” akasema Bw Nabwera.

“Pia nataka nafasi ya mgombea mwenza kwa sababu tuna idadi ya juu ya wapigakura pamoja na viongozi wenye uwezo wa kushika nafasi hiyo,” akaongeza.

Viongozi hao waliapa kuwa watafanya kampeni kali kuhakikisha Rais Ruto anapata kura za eneo la Magharibi.

Duru ziliarifu kuwa wakati wa mkutano, viongozi hao walimpendekeza mmoja kati ya Bw Mudavadi na Spika Wetang’ula awe mgombeaji mwenza wa Rais Ruto.

“Viongozi wote waliokuwepo waliwaidhinisha wawili hao kama wagombea wenza wanaopendelewa.

“Tumeapa kuungana na kusimama nao na hatutakubali juhudi zozote za kuwadharau au kuwavuruga,” duru hizo zikiaarifu.

Hatua hiyo inaonekana na wadadisi wa kisiasa kama mikakati ya kuwaengua Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya ambao umaarufu wao unaonekana umepanda sana eneo la Magharibi.

Bw Wetang’ula alisisitiza umuhimu wa umoja wa eneo hilo akisema kura zao zinatosha kumrejesha Rais Ruto mamlakani.

“Tuna idadi ya kutosha, tunachohitaji ni umoja,” akasema spika huyo.

Tangazo la Naivasha sasa linazidisha shinikizo kwa Rais akiwa na kibarua cha kumchagua mgombea mwenza wake.

Viongozi wengine wanaosemekana kumezea mate nafasi ya Prof Kindiki ni Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, Waziri wa Madini Hassan Joho na Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru.

Aidha, UDA sasa iko katika mazungumzo na ODM kuhusu muafaka wa uchaguzi mkuu wa mnamo 2027 na Rais ana kibarua cha kuamua wadhifa wa kutengea mrengo huo.

Bw Wetang’ula na Mudavadi wamekuwa katika uongozi wa jamii ya Mulembe kwa miaka mingi ila eneo hilo limesalia limegawanyika kinyume na ilivyokuwa enzi za aliyekuwa Makamu wa Rais Wamalwa Kijana.

Makamu wa Rais wa mwisho kutoka jamii ya Mulembe ni Moody Awuori ambaye alihudumu kati ya 2003-2007.