Masuala tisa yanayotatiza mrengo wa upinzani uchaguzi wa 2027
SIASA kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027 zimechukua mkondo mpya huku mrengo wa upinzani ukiwa na nafasi nzuri ya kumbwaga Rais William Ruto ikiwa itaungana na kumteua mgombea mmoja.
Rais Ruto anaingia katika kipindi cha mwisho wa muhula wake wa kwanza akiwa na muungano unaoshikiliwa zaidi na siasa za kuwavuta wapinzani serikalini kuliko misingi ya pamoja ya kisiasa.
Wakati huo huo, aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua anaendelea kumkosoa vikali huku kizazi kipya cha wapiga kura kilichochochewa na maandamano dhidi ya Mswada wa Fedha wa mwaka 2024 kikionekana kupoteza imani kwa serikali.
Lakini tatizo ni kuwa upinzani haujaonyesha umoja.
Kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa, viongozi wa upinzani wamekuwa wakijadili vigezo tisa vya kumpata mgombea wa pamoja bila kufikia makubaliano yoyote.
Kwa sasa, upinzani una makundi mawili yasiyosajiliwa rasmi.
Kundi la United Alternative Government linajumuisha Kalonzo Musyoka, Rigathi Gachagua, Martha Karua, Eugene Wamalwa na George Natembeya huku Linda Mwananchi likihusisha Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna ambaye pia anatajwa kuwa na uwezo wa kuwania urais.
Mipango ya viongozi hao kukutana kujadili mgombea mmoja imeahirishwa mara kadhaa huku Bw Gachagua akisema kutangaza mgombea mapema kutampa Rais Ruto nafasi ya kuharibu tiketi hiyo kisiasa.
Vigezo vilivyowekwa ni pamoja na ushirikishaji wa wananchi, tafiti za kisayansi, jinsia, umri na uzoefu, nguvu za kura katika maeneo mbalimbali, uwezo wa kuhamasisha wafuasi, uwezo wa kifedha, uadilifu na rekodi ya utendakazi.
Mchambuzi wa siasa Gasper Odhiambo anasema vigezo hivyo vinaonyesha kuwa si siri viongozi hao hawakubaliani.
“Kila mmoja tayari anaamini vigezo fulani vinamnufaisha yeye binafsi. Hii inaonyesha kuna mgogoro unaotokota,” alisema.
Bw Gachagua anasema yeye ndiye anayefaa zaidi kutokana na uwezo wake wa kuhamasisha watu, kukusanya fedha za kampeni na kuwa na ushawishi mkubwa eneo la Mlima Kenya.
Kwa upande wake, Kalonzo Musyoka amesema uzoefu wake wa zaidi ya miaka 15 ya kupambana na tawala mbalimbali unampa nafasi nzuri ya kuwa mgombea wa upinzani.
Utafiti wa Mizani Africa wa Desemba 2025 ulionyesha Kalonzo anaungwa mkono na asilimia 39.6 kitaifa huku akiwa na nguvu Nairobi, Rift Valley, Pwani na hata Mlima Kenya.
Aliyekuwa Waziri wa Usalama Fred Matiang’i anaonekana kuegemea kwenye hoja ya uadilifu, utendaji na uteuzi wa kisayansi.
Katika mahojiano na Taifa Leo, Dkt Matiang’i alisema mchakato wa kumpata mgombea unapaswa kuwa wa wazi, wa haki na unaotegemea data badala ya maamuzi ya viongozi wachache.
Rais mstaafu Uhuru Kenyatta amekuwa akimuunga mkono waziwazi akisema Matiang’i ana uwezo mkubwa wa kupambana na ufisadi ingawa si mwanasiasa wa kawaida.
Martha Karua naye amesema hakuna kiongozi anayepaswa kujiona bora kuliko wengine akisisitiza kuwa wote ni sawa ndani ya muungano huo.
Alisema anaamini Kenya iko tayari kupata rais mwanamke.
Lakini wachambuzi wanasema hoja kubwa inayowasumbua Wakenya wengi si umri wa wagombea wala uwezo wao wa kifedha, bali ni nani anaelewa matatizo ya wananchi wa kawaida.
Kura mpya kutoka kwa vijana inaonekana kubadilisha siasa za jadi zilizotegemea maeneo ya kikabila na viongozi wakongwe.
Swali kuu kwa wapiga kura wapya ni nani anaweza kushughulikia gharama ya maisha, ufisadi na uwajibikaji serikalini.